Thursday, August 6, 2015

JINSI GANI KIJANA !?. Sehemu ya 1



     Bwana Yesu Asifiwe, najua ni muda sijapost somo lolote hapa ndani, ni kwa sababu si kila mara napost isipokuwa tu Mungu anaponipa kitu cha kusema. Ebu shiriki na mimi somo hili jipya ambapo naamini litakujenga. Labda wewe ni kijana, mafunzo haya ni muhimu kwako, labda ni mzazi ama mlezi, itakusaidia kumtazama kijana unayemlea kwa jicho tofauti. Karibu.

Usijaribu kumpendeza kila mtu, kimsingi usijaribu kumpendeza mtu bali Mungu. Moja ya mambo ambayo yanawasumbua vijana wengi ni hali ya kutamani kukubalika na mtu ama watu katika jamii yao hata kama wanalazimika kujikosea katika kutimiza hilo. 

Mara nyingine jamii zetu, watu wanaotuzunguka na mara nyingine waliopaswa kutuongoza, wanatushawishi kuacha kile tunachojua kwamba ni sahihi, ili tufanye kile wanachodhani wao ndicho sahihi. Daudi alikumbana na hali hii. Wakati alipokwenda kuwatazama ndugu zake vitani, kaka zake hawakupenda yeye kwenda mstari wa mbele, hawakupenda yeye kuona wakishindwa vita, hawakupenda yeye kuona wakitusiwa na kudhalilishwa na Mfilisti, na hivyo wakalazimisha Daudi asisogee kwenye uwanja wa vita. 

Hawakujua kwamba Daudi pamoja na kwamba hakuwahi kupitia mafunzo ya kijeshi, alikuwa na mbinu za mapambano kwa kupambana na Simba na Dubu waliovamia mifugo yake machungani. Alikuwa na uwezo wa kuchukua kile alichojifunza kwenye maisha yake kwenye hatua fulani, na kukitumia kwenye hatua nyingine, na hivyo alikuwa na msaada. Walichokuwa wanakikosa askari wa Sauli ni morali ya vita na waliikosa kwa sababu kiongozi alikuwa ameacha msingi. Tutazungumza zaidi huko mbele juu ya kutambua kile kinachokufanya utiwe nguvu, kinachokufanya uwe tofauti, kinachokufanya utengwe na wenzako na kuonekana wa tofauti. Ukiacha asili ya nguvu zako, huwezi kupambana vitani na maisha ni vita. Imani ya Israel katika Mungu ndiyo ulikuwa msingi na asili ya ushindi wa watu vitani. Kama watu hawakuwa wakijua wanasimama wapi katika mahusiano yao na Mungu, basi hawakuwa na uwezo wa kupigana na adui. Daudi alikuwa tofauti. Daudi alikuwa na mahusiano thabiti na Mungu kwa namna yake. 

Sikia kauli yake anaposema “….BWANA aliyeniokoa na makucha ya Simba na makucha ya Dubu, ataniokoa na Mfilisti huyu…..” Daudi alikuwa na uzoefu si wa vita kwa mfumo wa kijeshi, lakini kwa vile alikuwa na tumaini ndani ya Mungu, alifahamu kwamba uzoefu wake ungetumika badala ya ujuzi kwa nafasi hii. 

Hakuwa akitafuta kumpendeza mtu, alikuwa akitafuta kushinda, kutumia yale anayoyajua kwa ajiri ya kupata hatua mpya katika maisha. Wakati kaka zake walikuwa wameridhika kutumika kwenye jeshi la Sauli, labda wakirudi nyumbani mara moja moja na kumletea mzee Yese zawadi kadha, na hata kuwashangaza watu wa  kijiji chao kwa mavazi yao ya kijeshI, Daudi alikuwa na lengo pana zaidi, “….kuifanya jamii yake kuwa huru katika Israel…….”. Samweli. 17:25 Ahadi ya mfalme kwa yeyote ambaye angemshinda Mfilisti ilikuwa “…mtu Yule atakayemuua, mfalme atamtajirisha kwa utajiri mwingi, naye atamwoza binti yake, na kuifanya mbari ya baba yake kuwa huru katika Israel”. Daudi hakuwa tayari kuacha maneno ya wale ambao waliridhika na mambo madogo, kumkosesha kile alichoamini Mungu amekiandaa kwa ajiri yake. 

Sasa hili halimaanishi kwamba uwe mkorofi tu na usiyefuata maongozi, lakini inakupasa uwe na hekima ya kutambua kuna nini nyuma ya kila unachokisikia na kukiona.
Ni kawaida ya vijana wengi kuwa na ndoto kubwa na mara nyingi tumepita kwenye mambo magumu yaliyotufanya kufikiri kwamba ikiwa Mungu hakuwa na lengo lolote na maisha yetu, kwanini ametupitisha kwenye mambo magumu namna hii? Ni sawa kuwaza hivi. Ndiyo. Kwa sababu kila unachokipitia katika maisha kama kijana, kinakuandaa kwa kule unakokwenda na utakavyokuwa pindi uwapo mtu mzima. 

Ni muhimu kwa kijana kujitambua. Ingawa kujitambua umekuwa msemo unaotumika sana kwenye jamii, lakini bado wengi wetu hawafahamu upana wa neno hili na mchango wa kujitambua kwao katika maisha ya kawaida. 

Wako wanaotafsiri kujitambua kuwa ni uwezo wa kwenda kwa kufuata utamaduni ama desturi za jamii waishiyo. Japokuwa tafsiri hii inaweza kuwa sehemu ya ukweli, lakini huu si ukweli wote maana kujitambua ni zaidi ya kutenda kwa namna inayokufanya kukubalika na jamii yako. Mara nyingi zaidi, kujitambua huweza kukufanya usikubalike na wengi kwenye jamii yako siyo kwa sababu wanakuchukia, bali kwa vile wanashindwa kukuelewa na binadamu ni kiumbe mgumu kuishi na mtu ama kitu asichokielewa. 

Kujitambua ni kufanyaje!?. Nasema kujitambua ni kujihoji na kupata majibu sahihi juu ya maswali matano kuhusu maisha yako. Maswali hayo ni;

 Je wewe ni Nani!?.
Watu wengi huamini kwamba wazazi ndiyo wanaokufahamu kuliko mtu mwingine yeyote na hili ni kweli, lakini wakati wa kuzaliwa kwako yawezekana (hasa kwa vile teknolojia ilikuwa bado duni) wazazi wako hata hawakujua ikiwa wewe ni mtoto wa kike ama wa kiume, hawakujua ikiwa una viungo vyako kamili ama una ulemavu fulani, hawakujua hata uzito wa mwili wako na kadhalika.
Ni vivyo hawakujua wewe ni nani, kusudi la kuzaliwa kwako ni nini na je utakuja kufanya nini katika maisha yako!?. Kwao wewe ulikuwa mtu mpya, mtu wa ajabu, na hivyo walikupa jina kutokana na hisia, imani ama desturi yao tu, walitimiza kwako wajibu wao kama wazazi wako wa kuhakikisha unapata mahitaji yako ya msingi na kadhalika huku wakijifunza jambo jipya kuhusu wewe karibu kila siku ya maisha yako. Ndiyo, walikufundisha mambo mengi, lakini kimsingi hawakuyaweka ama kuyaumba ndani yako mambo hayo, bali walikusaidia kuyagundua na kuyatumia bila kuleta madhara kwako na kwa wengine. Ebu fikiri mambo kama kuongea, kusogea, kutambua sura za watu, mvuto kati yako na watu wa karibu yako, upendo na kutafsiri matendo ya hisia za upendo kama kutabasamu na kucheka na kadhalika, mambo haya hukufunzwa na mtu, yalikuwamo ndani yako katika kuumbwa kwako. 

Ni kwa uwezo wa kimaumbile ulitambua matumizi ya viungo mbalimbali katika mwili wako. Hukusubiri kufundishwa matumizi ya kinywa kwa kula na kuongea, hukusubiri kufundishwa matumizi ya mikono katika kushika vitu na kadhalika. Pale tu uliposhindwa kutumia viungo ambavyo ulipaswa kuvitumia bila kufundishwa kufanya mambo ambayo wazazi wako kwa sababu ya uzoefu walijua unahitaji kuvitumia, ndipo walipofanya juhudi za utabibu kujua kuna tatizo gani kwamba baadhi ya viungo havitumiki ama huvitumii na kadhalika. 

Hiyo yote ni kusema hakuna mtu humu duniani anayekujua kama unavyojijua wewe mwenyewe na hata wewe hujijui kama anavyokujua Mungu muumbaji wako. 

Kwa hiyo, katika kujibu swali la wewe ni nani, kwanza unapaswa kuondokana na tafsiri za watu kuhusu wewe ni nani. Wakati Yesu alipoanza kusema na kufundisha, viongozi na hata watu wengine katika jamii yake walianza kutafuta kumfungia kwenye upana wa vile walivyokuwa wakimuona na hivyo si ajabu waliuliza; “…….huyu si mwana wa Seremala…….. na nduguze tunao hapa kwetu……….!?
 
Katika hatua hii ya kujitambua kama kijana kwa kujitafsiri wewe ni nani, inakupasa kujihadhari usijifungie kwenye tafsiri za watu waliokuzunguka.
Huwezi kutambua kusudi ama uwezo wa mashine yoyote bila kwanza kumsikiliza mtengenezaji wa mashine husika ama kusoma maelekezo yake kuhusu mashine hiyo. Vivyo wewe, huwezi kuutambua uwezo wako, vipawa vyako, mipaka yako na kadhalika isipokuwa utambuzi huo unatoka kwa mtengenezaji ama muumbaji wa wanadamu naye ni Mungu. Ndiyo maana mwandishi wa Zaburi anasema “…..kwa kutii akilifuata neno lako”  

Pengine unawaza kama yule kijana tajiri aliyemwambia Yesu “…..hayo yote nayajua na kuyafuata tangu ujana wangu….”. Uko sahihi, na ndiyo maana si lengo langu kukupa majibu ya moja kwa moja juu ya swali hili. Naweza kukwambia walau kwa usahihi wa kiwango fulani kwamba mimi ni nani, lakini siwezi kukwambia wewe ni nani. Ninaweza hata hivyo kukushawishi ujiulize swali hili kwa sababu ni muhimu sana. Ni swali ambalo litakufanya utafiti na kuhoji kila kitu kuhusu wewe, ni swali litakalokufanya uchunguze madhaifu yako na mazuri yako na kuyaweka yote kwenye mizani katika kutafuta majibu, na ni katika kufanya hivyo tu, unapoboresha uwezo wako wa kujipambanua na hivyo kujitambua. 

Ebu fikiri kwamba wakati ninapoandika maandishi haya, idadi ya watu duniani inafikia watu bilioni saba na kila mtu anavyo vitu kwenye vinasaba (DNA) vyake vinavyomtofautisha na mwingine. Alama zako za vidole hazifanani na za mtu yeyote yule duniani, mboni zako za macho zina tofauti na watu wengine wote duniani na hata mvumo wa sauti yako ni tofauti na watu wengine wote duniani. Hii maana yake ni kwamba wewe ni mtu tofauti na watu wengine wote waliowahi kuishi, wanaoishi na watakaoishi baada yako. Wewe ni maalumu sana. Tafuta kuutambua umaalumu wako. Inaaminika kwamba ujuzi sahihi huja kwa kuuliza maswali sahihi na mimi naamini pia katika kuuliza mahala sahihi, na majibu ya wewe ni nani yanaweza kutolewa na Mungu muumbaji peke yake. 

Hiyo haikuzuii hata hivyo kujisomea vitabu na tafiti kadhaa kuhusu watu wa aina yako hasa kwa sababu Kwanini ni swali ambalo limekuwapo kwa miaka dahali na litaendelea kuwapo. Sijaribu kukushawishi ujisomee Biblia ama vitabu na machapisho ya dini peke yake, maana kwa kufanya hivyo utakuwa umeshindwa kuyashindanisha mawazo na kushindanisha mawazo ndiyo hulka bora kabisa ya binadamu. 

Ninakushawishi ujisomee na kutafiti kwa kadri unavyoweza na kujiongezea maarifa katika kujitafakari, kuvumbua hazina za vipawa na karama vilivyomo ndani yako, kutafiti mahala na wakati unapoweza kutumia vipawa hivyo na kadhalika, lakini nakushauri ufanye hivyo ukiwa na msingi kwenye neno la Mungu maana kama ilivyo kwamba kila chombo kilichoundwa na mwanadamu kimeandikiwa namna ya matumizi yake, kadhalika Mungu ameandika kuhusu uumbaji wake na masharti ya matumizi yake. Tunapokiuka, tunatafuta madhara. 

Inaendelea......!

No comments:

Post a Comment