Sunday, August 9, 2015

JINSI GANI KIJANA!?- Sehemu ya 1 (2)



 Karibu. Tunaendelea na mfululizo wa somo letu juu ya Jinsi gani kijana aisafishe njia yake!? Kama utakavyoona huko mbeleni, kama hakuna "uchafu" kwenye njia, bila shaka Daudi asingetushauri kuzisafisha njia zetu. Na pia tusingehitaji kuzitambua na kuzisafisha njia kama hakuna tunakokwenda. Karibu, uendelee kujisomea.

 Kwanini niliumbwa?  
Swali la pili katika juhudi za kujitambua ni kwanini uliumbwa na kwanini umeumbwa ulivyoumbwa?. 

Kuna misemo mingi na maelezo mengi sana kuhusu kwanini. Kwanini huwa mwanzo wa  udadisi ama hasi au chanya kwa yule anayeuliza. Kwanini imekuwa chanzo cha vumbuzi nyingi tuzionazo duniani leo. Mtafiti na mwanasayansi aliyegundua mawasiliano ya simu, alisukumwa na kwanini asiweze kufikisha mazungumzo ya sauti umbali umbali mrefu zaidi na leo tunazo simu za viganjani, madaktari bingwa wa madawa ya utabibu na kemia husukumwa na kwanini katika kuanza tafiti zao ambazo huwa msaada mkubwa kwa matatizo ya binadamu na kadhalika. 

Hata kijana katika juhudi za kujitambua, yapaswa kujiuliza swali hili mara nyingi kwa kadri uwezavyo. Swali hili ndilo hufanya watu kusafiri mwendo mrefu, kufika mbali katika taaluma na kadhalika kwa kujihoji ni kwanini niliumbwa. 

Je! Niliumbwa ili nile, nilale, nijenge nyumba na kuishi ndani yake, niliumbwa niishi, nizeeke, nife, ama niliumbwa nifanye jambo fulani katika maisha yangu!?. 

Ili kujibu swali la kwanini uliumbwa, unahitaji kwanza kutambua mambo kadha wa kadha yanayokutofautisha na watu wengine. Katika maisha kila mtu anao uzoefu wake, uzoefu wako mpaka hapo ulipofika unaweza kukwambia mengi kuhusu wewe. Nakumbuka wakati nilipokuwa mdogo, nilipokuwa mdogo, nilipenda kukaa na kusikiliza mijadala ya watu wazima, na kwa vile nililelewa na bibi yangu ambaye hakusita kujibu swali lolote nililomuuliza, si ajabu nikiwa na umri wa miaka tisa tu nilihubiri somo langu la kwanza kwenye mkesha wa usiku mbele ya waumini wasiozidi ishirini. Kwangu hilo lilikuwa fanikio kubwa, miaka ishirini baadaye, nimeweza kuzungumza na umati wa watu kwenye maeneo mengi, nimekuwa kwenye mikutano kadha wa kadha yenye changamoto na watu wamesema vyema juu ya uzungumzaji wangu na sasa nimejifunza kwamba kumbe mimi ni msemaji. 

Ni pale nilipogundua kwamba watu wanalipwa mishahara mikubwa kuwa wasemaji wa taasisi kubwa duniani, nilipojifunza kwamba wahubiri wakubwa wanaishi maisha yao yote kwa kuzungumza na wanasiasa hufanikiwa katika siasa pamoja na mambo mengine, kwa kuwa wazungumzaji wazuri.
Ni baada ya utambuzi huo nilipoanza kujifunza namna ya kuboresha uwezo wangu wa kuzungumza, sijafanikiwa sana bado, lakini naweza kuzungumza na watu wengi, naweza kuwafanya watu wanisikilize kwa muda mrefu, naweza kujua wakati wasikilizaji wangu wanaponisikiliza kwa uvumilivu tu ama kwa kunielewa na shauku ya kuendelea kusikia. Ningali najifunza, lakini walau nimetambua jambo. 

Vivyo kwenye maeneo mengine, katika kujiuliza wewe ni nani unahitaji kufahamu baadhi ya mambo yanayokutofautisha na wengine na kukuhusianisha na wengine. 

Leo ninaandika makala na vitabu, lakini uandishi huu ni matokeo ya kupenda kujisomea vitu vingi. Sisubiri taarifa yoyote inifuate, naitafuta ikiwa ninaihitaji ama ninaitaka. Wakati nilipogundua kwamba nina tatizo la kujiamini mbele ya watu na kwamba hilo lilikuwa likininyima uwezo wa kuwa bora kwenye nafasi yangu, sikuwa na muda wa kwenda chuo kusomea lugha za alama lakini nilikuwa na uwezo wa kupakua kutoka mtandao vitabu vya wataalamu kadha wa kadha kuhusu somo husika, japo sijafaulu sana kwa jambo hili, lakini nimesaidika kwa sehemu kubwa. 

Najaribu kusema kwamba kama ambavyo mashine zote duniani zimetengenezwa zilivyotengenezwa kwa lengo moja tu la kuziwezesha kutekeleza lengo la kuundwa kwake, vivyo na wewe umeumbwa ulivyoumbwa kwa ajiri ya kutimiza kusudi fulani katika maisha.  Na kama tulivyoona hapo awali, ni rahisi kulijua lengo ama kazi ya mashine fulani kwa kuuliza ama kusoma maelekezo (Manual) ya mtengenezaji, na wewe muulize na soma neno la Mungu kwa ajiri ya kujua lengo la kuumbwa kwako hivyo ulivyoumbwa. 

Naona kama tatizo kubwa la vijana ni kutozilisha akili zao aina sahihi za vyakula. Kama hujui, chakula cha akili ni taarifa na unaweza kuilisha akili yako kwa vitu vingi sana ikiwamo televisheni, magazeti, vitabu na mitandao. Mara nyingi muonekano wa mwili wako husema sana ikiwa una afya ya kutosha ama lah! Na akili yako pia inao uwezo wa kusema ikiwa inayo afya ya kutosha ama lah!.
Unahitaji kula chakula bora, kupumzisha mwili wako, kuutunza kwa mavazi na kuuosha na kadhalika na haya twayafanya mara nyingi, lakini ni ajabu kwamba linapokuja suala la kuzilisha na kuzitunza akili zetu tunazembea. Vijana wengi hasa kwa vile miaka yao ya mwanzoni ya ujana huwakuta mashuleni na vyuoni, hudhani kwamba masomo ya shuleni yanatosha kuwafanya wao kuwa watu bora. Ndiyo, mitaala ya masomo imeandaliwa kukufanya kuwa mtaalamu wa jambo fulani, lakini bado unahitaji kujsomea vitu vingine kwa sababu utu wako unahusisha zaidi ya ufahamu wa kawaida ama intellect, unahitaji pia imani na “….imani huja kwa kusikia, na kusikia huja kwa neno la Kristo (Warumi 10:10), unahitaji hisia na kadhalika ili kuweza kushindana katika ulimwengu wenye mashindano mengi kama huu. 

Changamoto nyingine ni pale ambapo kijana amesomea kitu ambacho siyo kile alichonacho ndani ya utu na tabia yake. Wengi wa vijana hawana furaha japo wengine ni wasomi, wenye ajira nzuri na zenye kuwawezesha kulipia gharama muhimu za maisha yao na ziada. Ni changamoto kubwa Unapokuwa mtu anayependa kufundisha kama mimi, mtu anayependa kushirikiana na wengine kile anachokijua, mtu anayependa kuchunguza mambo ya kijamii na kujiuliza ama kutafiti ni kwanini jambo fulani katika jamii fulani liko vile na siyo hivi na kadhalika, lakini mtu huyu anashinda barabarani akijenga madaraja, ama akikadiria majengo ama akitengeneza mitambo na mashine. Mara zote pamoja na kwamba atafanikiwa kukamilisha kazi yake, atafanikiwa kumaliza ama kutimiza lengo la kazi husika, lakini hatopata ridhiko la moyo kwa vile hakutumia nguvu zake kutenda kile ambacho hasa humpa ridhiko kukifanya. 

Nilimuuliza Mhandisi mmoja juu ya aina fulani ya gari ambalo kwangu lilionekana kuwa na tabia ya ajabu kwa utumiaji wake wa mafuta. Ikiwa gari hilo litatumika kwa safari ndefu na kukimbia kwa mwendokasi mkubwa zaidi kidogo ya kawaida, matumizi yake ya mafuta huwa chini, kuliko likitumiwa katika barabara za mjini ambako mwendo wastani tu unatakiwa. Aliniambia gari hilo lilitengenezwa kwa ajiri ya mwendo kasi na siyo mwendo mdogo ama wa wastani na hivyo kwa sababu ya ukubwa wa injini yake, likiendeshwa kwa mwendo mdogo, halipati kufungua maeneo yote yanayopaswa na hivyo kulazimika kutumia nguvu nyingi kusukuma na hivyo kutumia mafuta mengi.
Mara nyingine umehisi kama maisha yako yako polepole na kwamba hayaendi kwa kasi ya kutosha!? Mara nyingine umehisi kama kile unachofanya katika maisha hakikupi ridhiko la moyo na hivyo, mara nyingi umehisi kama lile gari kwamba unatumia nguvu nyingi kuyasukuma maisha yako katika mwendo huu wa kuamka asubuhi, kwenda kazini kwako, kufanya kazi unazopangiwa ama zilizopangwa, kurudi nyumbani na kutazama televisheni na mara nyingine kuungana na rafiki zako kwenye mazungumzo na kadhalika, na unapoamka kesho yake maisha yako kama yalivyokuwa jana isipokuwa mabadiliko ya tarehe!?. Ndiyo, na huo ndiyo ukweli. Umeyaweka maisha yako kwenye mduara na ni vugumu kuona mambo ama maeneo mapya kama unazunguka kwenye duara. Ni pale tu unapofuata njia iliyonyooka kuelekea kule ambako unapaswa kwenda, ndipo unapopata nafasi ya kuona vitu vipya, kukutana na changamoto mpya njiani, kujifunza mambo mapya na kadhalika.
Ni kweli kwamba ni muhimu kwako kama kijana kuwa na ama kujenga nyumba, kuwa na familia na kusaidia ndugu na jamii yako, lakini safari yote ya maisha haiwezi kuwa tu inalenga huko! Wako wengi wetu ambao uhisi kama maisha yana maana zaidi ya kula na kulala, zaidi ya kuwa na kazi nzuri na mashahara mzuri na nyumba nzuri na mke ama mume mzuri na kadhalika. Ni kwa hawa mfalme Daudi aliandika na kuwashirikisha mawazo na maswali ya moyo wake aliposema “Ni jinsi gani kijana aisafishe njia yake………!?” hasa kwa sababu alitambua kwamba maisha ni zaidi ya kula na kulala bali ni safari. Siyo tu safari ya kuelekea mbinguni kama ambavyo tumeamini kwa miaka dahali, bali ni safari ya kuuishia ufalme wa Mungu. Ufalme ambao Mfalme wa ufalme huo Yesu Kristo hakuomba tuuendee, bali alitufundisha tuombe kwamba ufalme huo uje duniani. 

Sisemi tusijitunze kwa usafi wa moyo kwa ajiri ya maisha baada ya kifo, bali nasema kwa miaka tuliyomo duniani, yatupaswa kuuona utendaji wa ufalme wa Mungu kwenye maisha yetu ya kila siku na ufalme huo kama alivyosema Kristo, unakaa ndani yetu. Umemgundua mfalme aliyeko ndani yako!?. 

Wengi tunakumbuka jinsi ambavyo tulikuwa tukiambiwa tulipokuwa wadogo kwamba tulitakiwa kusubiri hadi tuwe wakubwa ndipo turuhusiwe kufanya mambo fulani. Bila shaka kulikuwa na hekima katika utaratibu huo, lakini kwa kadri siku zinavyokwenda, maisha na mifumo yake imerahisisha kufanya chochote unachoweza ama unachojisikia kufanya, almuradi huvunji sheria za nchi ama jamii yako. 

Hata hivyo, ukweli unabaki kwamba pana mambo ambayo hayahitaji tu uwezo ama ujuzi wa kuyafanya, bali kama asemavyo Mhubiri; “Pana wakati na majira kwa kila kusudi chini ya mbingu…..”

 Inaendelea.........!
Kwa maoni na ushauri, tume ujumbe wako kwenye Whatsup No. 0788653649 au email: kamengegm@yahoo.com 

No comments:

Post a Comment