Saturday, August 15, 2015

Jinsi Gani kijana kijana. 1 (4)



Ni kama mara nyingine Mungu hutumia mambo mabaya yanayotutokea kwenye maisha ili kutonyesha wito wetu hasa na kutuongoza kule ambako alitukusudia tangu kuwekwa misingi ya nchi. Tukiungana na Muhubiri kusema “Kwa kila jambo kuna majira yake, na wakati kwa kila kusudi chini ya mbingu”,(Mhubiri 3:1) tunapaswa kujifunza pia kwamba kuna changamoto zitokanazo na mabadiliko ya wakati na majira kwenye maisha yetu.
Moja ya changamoto ambazo zimenikabili mimi binafsi katika maisha yangu, ni kuvitambua na kuishi kwenye vipindi vya mpito. Kwa sababu mimi ni mtu ambaye nimeishi aina nyingi za maisha, nimejifunza kwamba mara nyingi wakati tunapokuwa hatuna jinsi yoyote isipokuwa kutumaini katika Mungu, huo ni wakati mgumu sana kwetu. Lakini huo ni wakati mzuri pia kwetu kwa sababu hutusaidia kuonyesha uwezo wa utu wetu. Mara nyingi nimejua moyoni mwangu kwamba hali ya mazingira ama mahusiano inaanza kubadilika hapa nilipo na kwamba ni wakati wa kwenda hatua nyingine, lakini hofu yangu ya kuacha kile nilichokizoea, kubadili lile ambalo ni kawaida na kuchukua hatua kwenye sintofahamu, kwangu hiyo huwa changamoto kubwa. Binafsi nimekuwa nikilazimishwa na Mungu kubadilika na usidhani imekuwa rahisi hasa wakati wa mchakato husika. Haikuwa rahisi kwa Musa. Kwanza alikuwa mtu aliyeishi kati ya mawazo mawili kwa muda mrefu sana, na alikuwa na utambulisho usioeleweka. Usingemtanabahisha kama Mmisri kwa sababu hakuwa Mmisri kwa kuzaliwa na bila shaka katika maisha yake ya kila siku alikuwa akiambiwa kwamba kama siyo tu kufadhiliwa na binti Farao, basi angekuwa huko Gosheni akifyatua matofali na Waebrania wenzie.
Ni ajabu lakini ukweli mchungu kwamba watu watakupokea kwenye kariba yao kama hawana budi isipokuwa wanalazimishwa kukupokea, lakini hawatakuacha kusahau wewe ni nani. Watatumia kila nafasi waipatayo kukumbusha kwamba hukustahili kuwa hapo, watatumia kila mapungufu yako kukusimanga na kukufanya ujisikie mnyonge, japo kwa wasiojua watakuona kuwa mtu mwenye furaha sana lakini siri ya moyo wako unaijua mwenyewe.
Nakumbuka jinsi nilivyoishi kwa shida kwenye nyumba ya mmoja wa ndugu zetu aliyekuwa mtu mkubwa na kiongozi wa serikali wakati huo. Nilikuwa nimetoka kijijini kwa ajiri ya kusoma eneo la mjini ambako mama yangu alikuwa akifanya kazi, lakini kwa sababu ya udogo wa nyumba aliyokuwa akiishi mama yangu, mimi nililazimika kwenda kuishi kwa huyo ndugu. Nilikuwa darasa la tatu na pale nyumbani kulikuwa na watoto wa darasa langu na wengine wakubwa kidogo. Wakati wa kula, mimi nilipaswa kusubiri kwanza wao wamalize kula ndipo na mimi nile. Sikuweza kula baadhi ya vyakula ambavyo vilihesabiwa kuwa vya anasa kama maziwa, juisi, nyama na kadhalika isipokuwa mara chache tu ikiwa mwenye nyumba alikuwampo, ambapo nilipata pia nafasi ya kukaa na familia nzima sebuleni kwa ajiri ya chakula na kutazama televisheni.
Kama mwenye nyumba hakuwapo, na kwa sababu ya kazi na nafasi yake alikuwa akisafiri sana, niliishi kila sekunde kama mtumwa, kila mara nikikumbushwa kwamba nilikuwa mshamba niliyetoka kijijini na nisiyestahili kutangamana na wao. Mambo hayo pamoja na kwamba yaliniumiza moyo, lakini yamenifanya kuwa makini na watu ambao Mungu ananipa nafasi ya kuwasaidia kwa lolote, nimemwomba Mungu anipe neema nisiseme lolote la kuwatweza maana nayajua maumivu yake. Nimejifunza kwamba watu hatuwezi kufanana kufikiri na kutenda kwetu na hivyo ikiwa tunaishi pamoja, basi kumbe itatupasa kuvumiliana sana.
Naona kama Musa naye alikuwa na wakati wa namna hii. Wanahistoria wa utawala wa Misri wa wakati huo wanasema baada ya kifo cha Farao, mmoja wa wana wa mfalme angeweza kuchukua nafasi ya kuwa Farao wa Misri. Hili nalo bila shaka liliongeza shida kwa Musa hasa kwa vile baadhi ya wanahistoria wanasema Musa alikuwa na uwezo maalumu katika mapigano na busara ya utawala kuliko wenzake na hivyo alipopata tuhuma ya kuua mtu, tena kutoka kwa watu wake mwenyewe, sasa alikuwa na wakati mgumu zaidi, adui zake walikuwa wamepata sababu ya kumshambulia zaidi. Lakini pia yasemekana Farao Tuthmosis II alimpenda Musa na sasa alikuwa njia panda. Si ajabu ambavyo hata waliokuwa rafiki zako kwenye mamlaka hugeuka kuwa adui zako wakati wa kujiliwa kwako ukifika!?. Si ajabu kwamba sifa ileile iliyokufanya kuajiriwa, ndiyo sifa hiyo hiyo inayokufanya leo wanatafuta kukuaa!?. Kwani si ujuzi wa mapigano na uwezo wa maamuzi wa Musa uliokuwa umempa sifa mbele ya Farao, lakini haki ilipodai kwamba Mmisri ashughulikiwe kwa uwezo ule ule, moto ukawaka na Musa akajikuta hana kwao?.
Tambua Changamoto za wakati wako au kwa kusema sahihi, tafuta wakati wako ndani ya changamoto zako maana Mungu hataruhusu jambo litokee kwako ambalo hujaweza kukabiliana nalo. Huu ulikuwa wakati wa Musa kusogea hatua nyingine na hii haikuwa hatua nzuri sana kwa Musa lakini ilikuwa sahihi, ya lazima kwa ajiri ya kusudi la Mungu. Kutoka Ikulu hadi katika Jangwa la Moabu, mwana wa mfalme aliyegeuka mchunga mbuzi. Bila shaka Wamisri wangecheka sana kwa kusikia habari hizi. Lakini ni kipawa chake hiki hiki cha maamuzi, moyo wa kupenda kuona haki, moyo wa kutoona wanyonge wakionewa, ndivyo vilivyomfikisha kwa Yethro. Ni vipawa vyake hivi hivi vilivyoendelea kumtengenezea njia hata kwenye hatua hii. Mapenzi yake ya kuona haki inatendeka.
Kut 3: 16-22 “Basi kuhani wa Midiani alikuwa na binti saba, nao wakaja wakateka maji, wakazijaza birika maji, wapate kunywesha kundi la baba yao.  Wachungaji wakaja wakawafukuza; lakini Musa akasimama, akawasaidia, akalinywesha kundi lao.  Walipofika kwa Reueli baba yao, akasema, Imekuwaje hata mkarejea mapema leo?  Wakasema, Mmisri mmoja alituokoa katika mikono ya wachungaji, tena zaidi ya hayo, akatutekea maji, akalinywesha kundi. Akawaambia binti zake, Yuko wapi basi? Mbona mmemwacha mtu huyo? Mwiteni, ale chakula.  Musa akawa radhi kukaa kwake mtu yule, naye akampa Musa binti yake, Sipora.  Huyo akamzalia mwana, akamwita jina lake Gershomu, maana alisema, Nimekuwa mgeni katika nchi ya ugeni”. 

Tukutane kwenye sehemu tatu za mwisho katika sura hii ya kwanza kuanzia juma lijalo. 

Tuesday, August 11, 2015

Jinsi Gani Kijana....!? Sehemu ya 1 (3)



Wakati tunapoaminishwa kwamba dunia kwa sasa inakwenda kasi kuliko wakati wowote na yawezekana ni kweli, na wakati tunapoambiwa na wataalamu wa tabia za binadamu kwamba uwezo wa akili na ubunifu wa mtu unapungua kwa kadri umri wake unavyoongezeka na hivyo kwamba mafanikio yana umri, hali halisi ni tofauti kabisa. 

Ukisoma Biblia utaona kwamba Musa aliyewakomboa Israel hakuanza kazi hiyo hadi alipokuwa na umri wa miaka themanini. Alitumia miaka arobaini ya kwanza ya maisha yake nyumbani mwa Farao akifundishwa jinsi ya kuwa na kuishi kama mtawala. Historia inaonyesha kwamba katika kizazi cha musa (Mnamo 1520BC) Misri ndilo taifa lililokuwa limestaarabika na likiitawala dunia, hawa ndiyo walikuwa mabingwa wa elimu, uchumi na utawala na Musa alizaliwa na kulelewa ndani ya ikulu ya utawala wa dunia wa wakati huo. Hii ni kusema Moses alikulia ikulu akifundishwa kufanya biashara, kupigana vita, kuamua mashauri na mafunzo mengine waliyofunzwa watoto wa ikulu ya farao Amunhotep I aliyeitawala Misri kati ya mwaka 1532-1511BC na Farao Tuthmosis II aliyetatufa kumuua Musa mnamo 1486 na hivyo Musa kulazimika kukimbia Misri. 

Wakati naisoma historia ya Musa, nikajifunza mambo kadhaa ambayo naona kama yana maana sana kwa kijana anayehangaika na suala la kujitambua na kuutambua wito wake katika maisha.
Navutwa kuamini kwamba siyo kweli kwamba Musa hakuifahamu historia yake hasa kwa kuzingatia kwamba alilelewa miaka yake ya awali ya utoto wake kwenye nyumba ya baba na mama yake ambao walikuwa Waebrania. Najua, nimesema hapo mwanzo kwamba Musa alikulia kwenye ikulu ya farao, lakini biblia iko wazi juu ya maisha ya utoto na msingi wa malezi ya Musa ulikuwa wapi. Kut: 2: 5-9.

  Basi binti Farao akashuka, aoge mtoni, na vijakazi wake wakatembea kando ya mto; naye akakiona kile kisafina katika majani, akamtuma kijakazi wake kwenda kukileta.  Akakifungua, akamwona mtoto, na tazama, mtoto yule analia. Basi akamhurumia, akasema, Huyu ni mmojawapo wa watoto wa Waebrania. Basi umbu lake mtoto akamwambia binti Farao, Je! Niende nikamwite mlezi katika wanawake wa Kiebrania, aje kwako, akunyonyeshee mtoto huyu? Binti Farao akamwambia, Haya! Enenda. Yule kijana akaenda akamwita mama yake yule mtoto.  Binti Farao akamwambia, Mchukue mtoto huyu, ukaninyonyeshee, nami nitakupa mshahara wako. Yule mwanamke akamtwaa mtoto, akamnyonyesha.  Mtoto akakua, naye akamleta kwa binti Farao, akawa mwanawe. Akamwita jina lake Musa, akasema, Ni kwa sababu nalimtoa majini”

Biblia inatwambia yule mtoto “akakua” lakini haisemi alikua kiasi gani na ni sahihi kufikiri kwamba wanawake wa kizazi kile walinyonyesha watoto muda mrefu kuliko leo, basi yawezekana kwamba Musa aliishi nyumbani kwa baba na mama yake muda mrefu sana. Lakini pia kwa sababu Musa na Haruni na Miriam wanaonekana kuwa na mahusiano imara hata wakati Musa aliporudi kutoka Midian, ingekuwa sawa kudhani kwamba upendo wao na makuzi yao wakati wa utoto ndivyo vitu vilivyojenga mahusiano haya wakiwa wakubwa. 

Lakini Biblia inatuonyesha kwamba “Hata siku zile, Musa alipokuwa mtu mzima, akatoka kuwaendea ndugu zake, akatazama mizigo yao……” Kutoka: 5:11. Mwandishi wa waraka kwa Waebrani analiweka sawa zaidi hil anaposema “….Musa alipokuwa mtu mzima, alikataa kuitwa mwana wa binti farao….”. Ebr 11

Biblia inasema Musa alipokuwa mtu mzima, aliamua kufanya maamuzi kadha wa kadha ambayo yalimpeleka kwenye wito wake katika maisha. Nilijifunza kupitia mstari huu kwamba Musa hakuanza kujitambua hadi alipofika umri wa miaka arobaini. Ni katika umri huu ambapo Musa anatoka na kwenda kuwatazama ndugu zake na labda hilo halikutarajiwa kwa mwana wa mfalme, labda pia kwa vile alikuwa ameasiwa kwenye familia ya kifalme na kila mmoja kwenye familia akijua kwamba hakuwa Mmisri, kwake yeye kuwatembelea Waebrania kulifanya wanausalama wa Misri kuchunguza mienendo yake zaidi?. Lakini Musa akijua kwamba yeye kuwatembelea waebrani inahatarisha maisha yake na nafasi yake, bado alitoka akaenda kuwatazama na alichokiona kikawasha moto uliokuwamo ndani yake muda mrefu. Moto wa kutotaka kuona Waebrania wakionewa, moto wa kutamani nao wawe watu huru, moto wa kutamani waishi na kuheshimiwa utu wao, ukawasha na ugomvi mdogo tu kati ya Mmisri na Muebrania. 

Ni jambo gani ambalo linakukera na unadhani ukipata nafasi utalibadili kabisa katika familia yako, katika jamii yako, katika taifa lako!?. Ni kitu gani ambacho ukikifanya katika jamii yako na kukikamilisha utajisikia umeishi maisha kwa ukamilifu? Kwa wengine ni kuwa daktari bingwa na kuweza kuwatibu watu aina fulani ya ugonjwa, kwa mwingine ni kuweza kujenga kiwanda cha kusindika mazao ya watu wake wanaoteseka na kulima bila kuwa na soko la mazao hayo, kwa mwingine ni kuwa hakimu ama mwanasheria kuwapa haki wanaoonewa na kwa mwingine ni kuwa kiongozi bora wa familia yake na kuwa mume bora na baba bora wa watoto wake na kadhalika. Kuna majira na wakati kwa jambo hilo na unaweza kuanza sasa. Yawezekana ukakosea mara kadhaa, yawezekana ukashindwa mara kadhaa na yawezekana katika kuanza ukajikuta umeharibu kabisa, lakini usiibadili talanta yako na ya mwingine, ama usiyapunguze maono yako kiasi cha kutafuta chakula na mavazi tu, una kitu cha ziada cha kufanya kuliko hayo. 

Kama unasoma makala haya, maana yake ni kwamba mimi walau nimefanikiwa kuandika na kuchapisha makala yenyewe, lakini huwezi kuamini ni vingapi havikufika hata kwa mchapishaji, ni vingapi hata sikuandika zaidi ya kurasa mbili, ni vingapi vilipotelea kwenye mikono ya watu nilioamini wangenisaidia kuvichapa na wao wakavitupa kwenye majalala kwa kuviona takataka.
Huwezi kujua ni makala ngapi niliandika na zilipotoka magazetini nikajiongezea maadui, huwezi kujua ni maandiko mangapi yalinifanya kupoteza marafiki, kufukuzwa kazi, kunyimwa nafasi kwenye maisha na kadhalika, lakini sikuacha kuandika. Sikuacha kuongea na watu hata kama walikuwa wawili tu, sikuacha kuanzisha mijadala iwe kwenye vyombo vya usafiri, kwenye nyumba za ibada, kwenye ofisi na mahala pa kazi, na hata mara nyingine nikihubiri na kuhutubia viti na meza sebleni kwangu kwa sababu nilikuwa na kitu cha kusema na haja ya kusikizwa.
Mpaka hapa nadhani tumeelewana kwamba kuna kusudi ndani ya kila mtu, kuna  talanta ama kipawa kilicho ndani yako. Nataka kurudi nyuma kidogo nikwambie mambo mawili kuhusu talanta na kisha twende kwenye swali linalofuata. 

Turudi kidogo kwenye habari za Musa aliyewatoa Israel kutoka utumwa wa Misri. Nimesema hapo mwanzo kwamba naamini alijifahamu kwamba kukulia kwake ndani ya ikulu ya Misri ilikuwa “bahati” tu hasa kwa vile alikuwa Mwebrania. Lakini yawezekana kwamba hakuwa na mkakati wowote wa kuwakomboa watu wale kutoka utumwa na hivyo pamoja na kuwahurumia, lakini hakuwa na kusudi la kuwaokoa wala hakuwa na mpango wowote. 

Unasema najuaje haya!? Kwanza kwa sababu ni pale tu “alipokuwa mtu mzima” (alipojitambua, alipojihoji na kuona lile shimo tupu  ndani ya moyo kwamba ajapokuwa anaishi kwa anasa kwenye jumba la kifalme lakini bado hakuwa na ridhiko halisi la moyo) ndipo alipoamua kujitanabahisha na watu wake hasa ambapo mwandishi wa waraka wa Waebrania anasema “…aliona ni sawa kuteseka na watu wa Mungu…..” Hii inamaanisha kwamba pamoja na kwamba alikuwa na nafasi, ujuzi na hata uwezo lakini alikuwa hajawa na utayari wa kuteseka na watu wake na hivyo aliona bora kula na kulala vizuri huku akiumia moyoni juu ya watu wake. 

Nimejifunza katika maisha yangu binafsi kwamba pana nyakati ambazo unaweza kuwa unafurahia kwa nje mazingira fulani ya raha uliyo nayo, lakini mazingira hayo hayakupi furaha wala riziko la moyo. 

Kuna wasichana wengi ambao wako kwenye mahusiano na wanaume watu wazima kuliko wao na labda waume za watu kwa sababu ya furaha ya kupewa fedha na kutimiziwa mahitaji yao kadhaa, lakini hawana ridhiko la moyo. Wana raha lakini hawana furaha. Ni ajabu pia kwamba wengi wa hawa, wana ujuzi na vipawa kadha wa kadha ambavyo vingewapa nafasi katika jamii yao na hata kuwafungulia milango ya kupata mahitaji yao, bila kulazimika kuwa watumwa.  Kuna vijana wengi walio kwenye matumizi ya madawa ya kulevya na kadhali kwa sababu wamekatishwa tamaa na muda wakidhani wamepitwa na wakati wao wamepitwa na muda wa kutumia vipawa vyao na katika ati kutafuta kujifariji, wamekuwa watumwa wa madawa ya kulevya na uharibifu wake.  

Nimesikia na kusoma juu ya wanawake wengi waliokuwa kwenye ndoa za mitala bila kutaka kwa vile tu walikuwa na mahitaji ama ya kiuchumi, ama ya kijamii kwa maana ya heshima na ulinzi wa kuwa na mume, mara wanawake hawa walipogundua nguvu ya maamuzi katika kumwamini na kumwishia Mungu, na maisha yao yamebadilika. 

Nilikutana na dada mmoja mkoani Tabora nchini Tanzania, yeye alikuwa binti mkristo ambaye aliamua kuolewa ndoa ya mitala kwa sababu ya hali ngumu ya uchumi na ugumu wa maisha. Alikaa kwenye ndoa hiyo kwa miaka zaidi ya saba hadi aliporudi kwa Kristo tena, hapo akaamua kwamba alikuwa na ndoto ya kuwa nesi maisha yake yote na kuamua kwenda kusomea unesi, leo mwanamke huyo ni nesi kwenye hospitali kuu ya mkoa, ameolewa na mwanaume wa ndoto zake na wana familia nzuri inayojiweza. Kifungo cha uchumi kimevunjwa na kutambua ndoto, kipawa na wito wa mwanamke huyu, wakati wa kuutekeleza na maamuzi ya kuanza na kufanya. 

Jambo la pili ni kuzielewa hatua za kujitambua. Kujitambua kwa mtu naweza kukufananisha na mfumo wa namna ambavyo kipepeo hubadilika kutoka Rava hadi kuwa mdudu mwenye mabawa na kupaa. Ni mchakato. Pia kujitambua hakuna mwisho kwa sababu ni ugunduzi wa uwezo uliomo ndani yako kwa nyakati tofauti za maisha. Unaweza kufanya kila kitu katika maisha, isipokuwa kwa aina na viwango tofauti kulingana na hatua uliyopo katika maisha.

  Musa hakuwa akiishi ikulu akijiandaa kutoka na kuwakomboa watu wake, aliishi na kutumikia utawala wa Misri na labda akitumaini siku moja kuwa mtawala wa Misri, hadi siku moja alipojaribu kuwasuruhisha waebrania waliokuwa wakigombana na kuishia kufukuzwa ndani ya Misri akiwa na mavazi yake tu. Labda aliwaza kuchukua kiti cha Misri siku moja na kisha kuwaachia Waebrania waende zao huku yeye akibakia Misri. Labda alijitia moyo kwa historia ya Yusufu ambaye japo hakuwa Mmisri, hakuwa amelelewa ikulu ya Misri, hakuwa na mafunzo ya utawala ya Kimisri, lakini alitawala Misri na katika utawala wake ndugu zake waliishi vizuri, lakini Mungu alikuwa na lengo tofauti kabisa.
Kutoka 2: 11-15 “Hata siku zile, Musa alipokuwa mtu mzima, akatoka kuwaendea ndugu zake, akatazama mizigo yao. Akamwona Mmisri anampiga Mwebrania, mmojawapo wa ndugu zake. Basi akatazama huko na huko, na alipoona ya kuwa hapana mtu, akampiga Mmisri yule, akamficha ndani ya mchanga.  Akatoka siku ya pili, na tazama, watu wawili wa Waebrania walikuwa wakipigana. Akamwambia yule aliyemdhulumu mwenzake, Mbona unampiga mwenzako?  Yule akasema, Ni nani aliyekuweka wewe kuwa mkuu wetu, na mwamuzi juu yetu? Je! Wataka kuniua mimi kama ulivyomwua yule Mmisri? Musa akaogopa, akasema, Kumbe! Jambo lile limejulikana. Basi Farao alipopata habari, akataka kumwua Musa; lakini Musa akakimbia mbele ya Farao, akakaa katika nchi ya Midiani; akaketi karibu na kisima” 

Inaendelea.......!!!!

Sunday, August 9, 2015

JINSI GANI KIJANA!?- Sehemu ya 1 (2)



 Karibu. Tunaendelea na mfululizo wa somo letu juu ya Jinsi gani kijana aisafishe njia yake!? Kama utakavyoona huko mbeleni, kama hakuna "uchafu" kwenye njia, bila shaka Daudi asingetushauri kuzisafisha njia zetu. Na pia tusingehitaji kuzitambua na kuzisafisha njia kama hakuna tunakokwenda. Karibu, uendelee kujisomea.

 Kwanini niliumbwa?  
Swali la pili katika juhudi za kujitambua ni kwanini uliumbwa na kwanini umeumbwa ulivyoumbwa?. 

Kuna misemo mingi na maelezo mengi sana kuhusu kwanini. Kwanini huwa mwanzo wa  udadisi ama hasi au chanya kwa yule anayeuliza. Kwanini imekuwa chanzo cha vumbuzi nyingi tuzionazo duniani leo. Mtafiti na mwanasayansi aliyegundua mawasiliano ya simu, alisukumwa na kwanini asiweze kufikisha mazungumzo ya sauti umbali umbali mrefu zaidi na leo tunazo simu za viganjani, madaktari bingwa wa madawa ya utabibu na kemia husukumwa na kwanini katika kuanza tafiti zao ambazo huwa msaada mkubwa kwa matatizo ya binadamu na kadhalika. 

Hata kijana katika juhudi za kujitambua, yapaswa kujiuliza swali hili mara nyingi kwa kadri uwezavyo. Swali hili ndilo hufanya watu kusafiri mwendo mrefu, kufika mbali katika taaluma na kadhalika kwa kujihoji ni kwanini niliumbwa. 

Je! Niliumbwa ili nile, nilale, nijenge nyumba na kuishi ndani yake, niliumbwa niishi, nizeeke, nife, ama niliumbwa nifanye jambo fulani katika maisha yangu!?. 

Ili kujibu swali la kwanini uliumbwa, unahitaji kwanza kutambua mambo kadha wa kadha yanayokutofautisha na watu wengine. Katika maisha kila mtu anao uzoefu wake, uzoefu wako mpaka hapo ulipofika unaweza kukwambia mengi kuhusu wewe. Nakumbuka wakati nilipokuwa mdogo, nilipokuwa mdogo, nilipenda kukaa na kusikiliza mijadala ya watu wazima, na kwa vile nililelewa na bibi yangu ambaye hakusita kujibu swali lolote nililomuuliza, si ajabu nikiwa na umri wa miaka tisa tu nilihubiri somo langu la kwanza kwenye mkesha wa usiku mbele ya waumini wasiozidi ishirini. Kwangu hilo lilikuwa fanikio kubwa, miaka ishirini baadaye, nimeweza kuzungumza na umati wa watu kwenye maeneo mengi, nimekuwa kwenye mikutano kadha wa kadha yenye changamoto na watu wamesema vyema juu ya uzungumzaji wangu na sasa nimejifunza kwamba kumbe mimi ni msemaji. 

Ni pale nilipogundua kwamba watu wanalipwa mishahara mikubwa kuwa wasemaji wa taasisi kubwa duniani, nilipojifunza kwamba wahubiri wakubwa wanaishi maisha yao yote kwa kuzungumza na wanasiasa hufanikiwa katika siasa pamoja na mambo mengine, kwa kuwa wazungumzaji wazuri.
Ni baada ya utambuzi huo nilipoanza kujifunza namna ya kuboresha uwezo wangu wa kuzungumza, sijafanikiwa sana bado, lakini naweza kuzungumza na watu wengi, naweza kuwafanya watu wanisikilize kwa muda mrefu, naweza kujua wakati wasikilizaji wangu wanaponisikiliza kwa uvumilivu tu ama kwa kunielewa na shauku ya kuendelea kusikia. Ningali najifunza, lakini walau nimetambua jambo. 

Vivyo kwenye maeneo mengine, katika kujiuliza wewe ni nani unahitaji kufahamu baadhi ya mambo yanayokutofautisha na wengine na kukuhusianisha na wengine. 

Leo ninaandika makala na vitabu, lakini uandishi huu ni matokeo ya kupenda kujisomea vitu vingi. Sisubiri taarifa yoyote inifuate, naitafuta ikiwa ninaihitaji ama ninaitaka. Wakati nilipogundua kwamba nina tatizo la kujiamini mbele ya watu na kwamba hilo lilikuwa likininyima uwezo wa kuwa bora kwenye nafasi yangu, sikuwa na muda wa kwenda chuo kusomea lugha za alama lakini nilikuwa na uwezo wa kupakua kutoka mtandao vitabu vya wataalamu kadha wa kadha kuhusu somo husika, japo sijafaulu sana kwa jambo hili, lakini nimesaidika kwa sehemu kubwa. 

Najaribu kusema kwamba kama ambavyo mashine zote duniani zimetengenezwa zilivyotengenezwa kwa lengo moja tu la kuziwezesha kutekeleza lengo la kuundwa kwake, vivyo na wewe umeumbwa ulivyoumbwa kwa ajiri ya kutimiza kusudi fulani katika maisha.  Na kama tulivyoona hapo awali, ni rahisi kulijua lengo ama kazi ya mashine fulani kwa kuuliza ama kusoma maelekezo (Manual) ya mtengenezaji, na wewe muulize na soma neno la Mungu kwa ajiri ya kujua lengo la kuumbwa kwako hivyo ulivyoumbwa. 

Naona kama tatizo kubwa la vijana ni kutozilisha akili zao aina sahihi za vyakula. Kama hujui, chakula cha akili ni taarifa na unaweza kuilisha akili yako kwa vitu vingi sana ikiwamo televisheni, magazeti, vitabu na mitandao. Mara nyingi muonekano wa mwili wako husema sana ikiwa una afya ya kutosha ama lah! Na akili yako pia inao uwezo wa kusema ikiwa inayo afya ya kutosha ama lah!.
Unahitaji kula chakula bora, kupumzisha mwili wako, kuutunza kwa mavazi na kuuosha na kadhalika na haya twayafanya mara nyingi, lakini ni ajabu kwamba linapokuja suala la kuzilisha na kuzitunza akili zetu tunazembea. Vijana wengi hasa kwa vile miaka yao ya mwanzoni ya ujana huwakuta mashuleni na vyuoni, hudhani kwamba masomo ya shuleni yanatosha kuwafanya wao kuwa watu bora. Ndiyo, mitaala ya masomo imeandaliwa kukufanya kuwa mtaalamu wa jambo fulani, lakini bado unahitaji kujsomea vitu vingine kwa sababu utu wako unahusisha zaidi ya ufahamu wa kawaida ama intellect, unahitaji pia imani na “….imani huja kwa kusikia, na kusikia huja kwa neno la Kristo (Warumi 10:10), unahitaji hisia na kadhalika ili kuweza kushindana katika ulimwengu wenye mashindano mengi kama huu. 

Changamoto nyingine ni pale ambapo kijana amesomea kitu ambacho siyo kile alichonacho ndani ya utu na tabia yake. Wengi wa vijana hawana furaha japo wengine ni wasomi, wenye ajira nzuri na zenye kuwawezesha kulipia gharama muhimu za maisha yao na ziada. Ni changamoto kubwa Unapokuwa mtu anayependa kufundisha kama mimi, mtu anayependa kushirikiana na wengine kile anachokijua, mtu anayependa kuchunguza mambo ya kijamii na kujiuliza ama kutafiti ni kwanini jambo fulani katika jamii fulani liko vile na siyo hivi na kadhalika, lakini mtu huyu anashinda barabarani akijenga madaraja, ama akikadiria majengo ama akitengeneza mitambo na mashine. Mara zote pamoja na kwamba atafanikiwa kukamilisha kazi yake, atafanikiwa kumaliza ama kutimiza lengo la kazi husika, lakini hatopata ridhiko la moyo kwa vile hakutumia nguvu zake kutenda kile ambacho hasa humpa ridhiko kukifanya. 

Nilimuuliza Mhandisi mmoja juu ya aina fulani ya gari ambalo kwangu lilionekana kuwa na tabia ya ajabu kwa utumiaji wake wa mafuta. Ikiwa gari hilo litatumika kwa safari ndefu na kukimbia kwa mwendokasi mkubwa zaidi kidogo ya kawaida, matumizi yake ya mafuta huwa chini, kuliko likitumiwa katika barabara za mjini ambako mwendo wastani tu unatakiwa. Aliniambia gari hilo lilitengenezwa kwa ajiri ya mwendo kasi na siyo mwendo mdogo ama wa wastani na hivyo kwa sababu ya ukubwa wa injini yake, likiendeshwa kwa mwendo mdogo, halipati kufungua maeneo yote yanayopaswa na hivyo kulazimika kutumia nguvu nyingi kusukuma na hivyo kutumia mafuta mengi.
Mara nyingine umehisi kama maisha yako yako polepole na kwamba hayaendi kwa kasi ya kutosha!? Mara nyingine umehisi kama kile unachofanya katika maisha hakikupi ridhiko la moyo na hivyo, mara nyingi umehisi kama lile gari kwamba unatumia nguvu nyingi kuyasukuma maisha yako katika mwendo huu wa kuamka asubuhi, kwenda kazini kwako, kufanya kazi unazopangiwa ama zilizopangwa, kurudi nyumbani na kutazama televisheni na mara nyingine kuungana na rafiki zako kwenye mazungumzo na kadhalika, na unapoamka kesho yake maisha yako kama yalivyokuwa jana isipokuwa mabadiliko ya tarehe!?. Ndiyo, na huo ndiyo ukweli. Umeyaweka maisha yako kwenye mduara na ni vugumu kuona mambo ama maeneo mapya kama unazunguka kwenye duara. Ni pale tu unapofuata njia iliyonyooka kuelekea kule ambako unapaswa kwenda, ndipo unapopata nafasi ya kuona vitu vipya, kukutana na changamoto mpya njiani, kujifunza mambo mapya na kadhalika.
Ni kweli kwamba ni muhimu kwako kama kijana kuwa na ama kujenga nyumba, kuwa na familia na kusaidia ndugu na jamii yako, lakini safari yote ya maisha haiwezi kuwa tu inalenga huko! Wako wengi wetu ambao uhisi kama maisha yana maana zaidi ya kula na kulala, zaidi ya kuwa na kazi nzuri na mashahara mzuri na nyumba nzuri na mke ama mume mzuri na kadhalika. Ni kwa hawa mfalme Daudi aliandika na kuwashirikisha mawazo na maswali ya moyo wake aliposema “Ni jinsi gani kijana aisafishe njia yake………!?” hasa kwa sababu alitambua kwamba maisha ni zaidi ya kula na kulala bali ni safari. Siyo tu safari ya kuelekea mbinguni kama ambavyo tumeamini kwa miaka dahali, bali ni safari ya kuuishia ufalme wa Mungu. Ufalme ambao Mfalme wa ufalme huo Yesu Kristo hakuomba tuuendee, bali alitufundisha tuombe kwamba ufalme huo uje duniani. 

Sisemi tusijitunze kwa usafi wa moyo kwa ajiri ya maisha baada ya kifo, bali nasema kwa miaka tuliyomo duniani, yatupaswa kuuona utendaji wa ufalme wa Mungu kwenye maisha yetu ya kila siku na ufalme huo kama alivyosema Kristo, unakaa ndani yetu. Umemgundua mfalme aliyeko ndani yako!?. 

Wengi tunakumbuka jinsi ambavyo tulikuwa tukiambiwa tulipokuwa wadogo kwamba tulitakiwa kusubiri hadi tuwe wakubwa ndipo turuhusiwe kufanya mambo fulani. Bila shaka kulikuwa na hekima katika utaratibu huo, lakini kwa kadri siku zinavyokwenda, maisha na mifumo yake imerahisisha kufanya chochote unachoweza ama unachojisikia kufanya, almuradi huvunji sheria za nchi ama jamii yako. 

Hata hivyo, ukweli unabaki kwamba pana mambo ambayo hayahitaji tu uwezo ama ujuzi wa kuyafanya, bali kama asemavyo Mhubiri; “Pana wakati na majira kwa kila kusudi chini ya mbingu…..”

 Inaendelea.........!
Kwa maoni na ushauri, tume ujumbe wako kwenye Whatsup No. 0788653649 au email: kamengegm@yahoo.com 

Thursday, August 6, 2015

JINSI GANI KIJANA !?. Sehemu ya 1



     Bwana Yesu Asifiwe, najua ni muda sijapost somo lolote hapa ndani, ni kwa sababu si kila mara napost isipokuwa tu Mungu anaponipa kitu cha kusema. Ebu shiriki na mimi somo hili jipya ambapo naamini litakujenga. Labda wewe ni kijana, mafunzo haya ni muhimu kwako, labda ni mzazi ama mlezi, itakusaidia kumtazama kijana unayemlea kwa jicho tofauti. Karibu.

Usijaribu kumpendeza kila mtu, kimsingi usijaribu kumpendeza mtu bali Mungu. Moja ya mambo ambayo yanawasumbua vijana wengi ni hali ya kutamani kukubalika na mtu ama watu katika jamii yao hata kama wanalazimika kujikosea katika kutimiza hilo. 

Mara nyingine jamii zetu, watu wanaotuzunguka na mara nyingine waliopaswa kutuongoza, wanatushawishi kuacha kile tunachojua kwamba ni sahihi, ili tufanye kile wanachodhani wao ndicho sahihi. Daudi alikumbana na hali hii. Wakati alipokwenda kuwatazama ndugu zake vitani, kaka zake hawakupenda yeye kwenda mstari wa mbele, hawakupenda yeye kuona wakishindwa vita, hawakupenda yeye kuona wakitusiwa na kudhalilishwa na Mfilisti, na hivyo wakalazimisha Daudi asisogee kwenye uwanja wa vita. 

Hawakujua kwamba Daudi pamoja na kwamba hakuwahi kupitia mafunzo ya kijeshi, alikuwa na mbinu za mapambano kwa kupambana na Simba na Dubu waliovamia mifugo yake machungani. Alikuwa na uwezo wa kuchukua kile alichojifunza kwenye maisha yake kwenye hatua fulani, na kukitumia kwenye hatua nyingine, na hivyo alikuwa na msaada. Walichokuwa wanakikosa askari wa Sauli ni morali ya vita na waliikosa kwa sababu kiongozi alikuwa ameacha msingi. Tutazungumza zaidi huko mbele juu ya kutambua kile kinachokufanya utiwe nguvu, kinachokufanya uwe tofauti, kinachokufanya utengwe na wenzako na kuonekana wa tofauti. Ukiacha asili ya nguvu zako, huwezi kupambana vitani na maisha ni vita. Imani ya Israel katika Mungu ndiyo ulikuwa msingi na asili ya ushindi wa watu vitani. Kama watu hawakuwa wakijua wanasimama wapi katika mahusiano yao na Mungu, basi hawakuwa na uwezo wa kupigana na adui. Daudi alikuwa tofauti. Daudi alikuwa na mahusiano thabiti na Mungu kwa namna yake. 

Sikia kauli yake anaposema “….BWANA aliyeniokoa na makucha ya Simba na makucha ya Dubu, ataniokoa na Mfilisti huyu…..” Daudi alikuwa na uzoefu si wa vita kwa mfumo wa kijeshi, lakini kwa vile alikuwa na tumaini ndani ya Mungu, alifahamu kwamba uzoefu wake ungetumika badala ya ujuzi kwa nafasi hii. 

Hakuwa akitafuta kumpendeza mtu, alikuwa akitafuta kushinda, kutumia yale anayoyajua kwa ajiri ya kupata hatua mpya katika maisha. Wakati kaka zake walikuwa wameridhika kutumika kwenye jeshi la Sauli, labda wakirudi nyumbani mara moja moja na kumletea mzee Yese zawadi kadha, na hata kuwashangaza watu wa  kijiji chao kwa mavazi yao ya kijeshI, Daudi alikuwa na lengo pana zaidi, “….kuifanya jamii yake kuwa huru katika Israel…….”. Samweli. 17:25 Ahadi ya mfalme kwa yeyote ambaye angemshinda Mfilisti ilikuwa “…mtu Yule atakayemuua, mfalme atamtajirisha kwa utajiri mwingi, naye atamwoza binti yake, na kuifanya mbari ya baba yake kuwa huru katika Israel”. Daudi hakuwa tayari kuacha maneno ya wale ambao waliridhika na mambo madogo, kumkosesha kile alichoamini Mungu amekiandaa kwa ajiri yake. 

Sasa hili halimaanishi kwamba uwe mkorofi tu na usiyefuata maongozi, lakini inakupasa uwe na hekima ya kutambua kuna nini nyuma ya kila unachokisikia na kukiona.
Ni kawaida ya vijana wengi kuwa na ndoto kubwa na mara nyingi tumepita kwenye mambo magumu yaliyotufanya kufikiri kwamba ikiwa Mungu hakuwa na lengo lolote na maisha yetu, kwanini ametupitisha kwenye mambo magumu namna hii? Ni sawa kuwaza hivi. Ndiyo. Kwa sababu kila unachokipitia katika maisha kama kijana, kinakuandaa kwa kule unakokwenda na utakavyokuwa pindi uwapo mtu mzima. 

Ni muhimu kwa kijana kujitambua. Ingawa kujitambua umekuwa msemo unaotumika sana kwenye jamii, lakini bado wengi wetu hawafahamu upana wa neno hili na mchango wa kujitambua kwao katika maisha ya kawaida. 

Wako wanaotafsiri kujitambua kuwa ni uwezo wa kwenda kwa kufuata utamaduni ama desturi za jamii waishiyo. Japokuwa tafsiri hii inaweza kuwa sehemu ya ukweli, lakini huu si ukweli wote maana kujitambua ni zaidi ya kutenda kwa namna inayokufanya kukubalika na jamii yako. Mara nyingi zaidi, kujitambua huweza kukufanya usikubalike na wengi kwenye jamii yako siyo kwa sababu wanakuchukia, bali kwa vile wanashindwa kukuelewa na binadamu ni kiumbe mgumu kuishi na mtu ama kitu asichokielewa. 

Kujitambua ni kufanyaje!?. Nasema kujitambua ni kujihoji na kupata majibu sahihi juu ya maswali matano kuhusu maisha yako. Maswali hayo ni;

 Je wewe ni Nani!?.
Watu wengi huamini kwamba wazazi ndiyo wanaokufahamu kuliko mtu mwingine yeyote na hili ni kweli, lakini wakati wa kuzaliwa kwako yawezekana (hasa kwa vile teknolojia ilikuwa bado duni) wazazi wako hata hawakujua ikiwa wewe ni mtoto wa kike ama wa kiume, hawakujua ikiwa una viungo vyako kamili ama una ulemavu fulani, hawakujua hata uzito wa mwili wako na kadhalika.
Ni vivyo hawakujua wewe ni nani, kusudi la kuzaliwa kwako ni nini na je utakuja kufanya nini katika maisha yako!?. Kwao wewe ulikuwa mtu mpya, mtu wa ajabu, na hivyo walikupa jina kutokana na hisia, imani ama desturi yao tu, walitimiza kwako wajibu wao kama wazazi wako wa kuhakikisha unapata mahitaji yako ya msingi na kadhalika huku wakijifunza jambo jipya kuhusu wewe karibu kila siku ya maisha yako. Ndiyo, walikufundisha mambo mengi, lakini kimsingi hawakuyaweka ama kuyaumba ndani yako mambo hayo, bali walikusaidia kuyagundua na kuyatumia bila kuleta madhara kwako na kwa wengine. Ebu fikiri mambo kama kuongea, kusogea, kutambua sura za watu, mvuto kati yako na watu wa karibu yako, upendo na kutafsiri matendo ya hisia za upendo kama kutabasamu na kucheka na kadhalika, mambo haya hukufunzwa na mtu, yalikuwamo ndani yako katika kuumbwa kwako. 

Ni kwa uwezo wa kimaumbile ulitambua matumizi ya viungo mbalimbali katika mwili wako. Hukusubiri kufundishwa matumizi ya kinywa kwa kula na kuongea, hukusubiri kufundishwa matumizi ya mikono katika kushika vitu na kadhalika. Pale tu uliposhindwa kutumia viungo ambavyo ulipaswa kuvitumia bila kufundishwa kufanya mambo ambayo wazazi wako kwa sababu ya uzoefu walijua unahitaji kuvitumia, ndipo walipofanya juhudi za utabibu kujua kuna tatizo gani kwamba baadhi ya viungo havitumiki ama huvitumii na kadhalika. 

Hiyo yote ni kusema hakuna mtu humu duniani anayekujua kama unavyojijua wewe mwenyewe na hata wewe hujijui kama anavyokujua Mungu muumbaji wako. 

Kwa hiyo, katika kujibu swali la wewe ni nani, kwanza unapaswa kuondokana na tafsiri za watu kuhusu wewe ni nani. Wakati Yesu alipoanza kusema na kufundisha, viongozi na hata watu wengine katika jamii yake walianza kutafuta kumfungia kwenye upana wa vile walivyokuwa wakimuona na hivyo si ajabu waliuliza; “…….huyu si mwana wa Seremala…….. na nduguze tunao hapa kwetu……….!?
 
Katika hatua hii ya kujitambua kama kijana kwa kujitafsiri wewe ni nani, inakupasa kujihadhari usijifungie kwenye tafsiri za watu waliokuzunguka.
Huwezi kutambua kusudi ama uwezo wa mashine yoyote bila kwanza kumsikiliza mtengenezaji wa mashine husika ama kusoma maelekezo yake kuhusu mashine hiyo. Vivyo wewe, huwezi kuutambua uwezo wako, vipawa vyako, mipaka yako na kadhalika isipokuwa utambuzi huo unatoka kwa mtengenezaji ama muumbaji wa wanadamu naye ni Mungu. Ndiyo maana mwandishi wa Zaburi anasema “…..kwa kutii akilifuata neno lako”  

Pengine unawaza kama yule kijana tajiri aliyemwambia Yesu “…..hayo yote nayajua na kuyafuata tangu ujana wangu….”. Uko sahihi, na ndiyo maana si lengo langu kukupa majibu ya moja kwa moja juu ya swali hili. Naweza kukwambia walau kwa usahihi wa kiwango fulani kwamba mimi ni nani, lakini siwezi kukwambia wewe ni nani. Ninaweza hata hivyo kukushawishi ujiulize swali hili kwa sababu ni muhimu sana. Ni swali ambalo litakufanya utafiti na kuhoji kila kitu kuhusu wewe, ni swali litakalokufanya uchunguze madhaifu yako na mazuri yako na kuyaweka yote kwenye mizani katika kutafuta majibu, na ni katika kufanya hivyo tu, unapoboresha uwezo wako wa kujipambanua na hivyo kujitambua. 

Ebu fikiri kwamba wakati ninapoandika maandishi haya, idadi ya watu duniani inafikia watu bilioni saba na kila mtu anavyo vitu kwenye vinasaba (DNA) vyake vinavyomtofautisha na mwingine. Alama zako za vidole hazifanani na za mtu yeyote yule duniani, mboni zako za macho zina tofauti na watu wengine wote duniani na hata mvumo wa sauti yako ni tofauti na watu wengine wote duniani. Hii maana yake ni kwamba wewe ni mtu tofauti na watu wengine wote waliowahi kuishi, wanaoishi na watakaoishi baada yako. Wewe ni maalumu sana. Tafuta kuutambua umaalumu wako. Inaaminika kwamba ujuzi sahihi huja kwa kuuliza maswali sahihi na mimi naamini pia katika kuuliza mahala sahihi, na majibu ya wewe ni nani yanaweza kutolewa na Mungu muumbaji peke yake. 

Hiyo haikuzuii hata hivyo kujisomea vitabu na tafiti kadhaa kuhusu watu wa aina yako hasa kwa sababu Kwanini ni swali ambalo limekuwapo kwa miaka dahali na litaendelea kuwapo. Sijaribu kukushawishi ujisomee Biblia ama vitabu na machapisho ya dini peke yake, maana kwa kufanya hivyo utakuwa umeshindwa kuyashindanisha mawazo na kushindanisha mawazo ndiyo hulka bora kabisa ya binadamu. 

Ninakushawishi ujisomee na kutafiti kwa kadri unavyoweza na kujiongezea maarifa katika kujitafakari, kuvumbua hazina za vipawa na karama vilivyomo ndani yako, kutafiti mahala na wakati unapoweza kutumia vipawa hivyo na kadhalika, lakini nakushauri ufanye hivyo ukiwa na msingi kwenye neno la Mungu maana kama ilivyo kwamba kila chombo kilichoundwa na mwanadamu kimeandikiwa namna ya matumizi yake, kadhalika Mungu ameandika kuhusu uumbaji wake na masharti ya matumizi yake. Tunapokiuka, tunatafuta madhara. 

Inaendelea......!