Tuesday, September 10, 2013

Wakati wa Kujaribiwa: Sura ya Kwanza, Sehemu ya Pili.



(1)  Aina za Majaribu
Majaribu yote hayako kwenye kundi moja tu. Ziko aina kadhaa za majaribu na hapa tutataja aina kuu tatu za majaribu ambazo ni:
(i)              Majaribu yatokanayo na Tamaa  binafsi za mjaribiwa.
Hii ni aina ya majaribu ambayo mjaribu anategemea hali na mazingira yetu kabla hajatujaribu. Yak 1:12- 14.
Pamekuwa na makosa ya tafsiri kuhusu andiko hili ambalo mzee Yohana anatuandikia kutuonya juu ya kujaribiwa na tamaa zetu. Watafsiri wengi wamelifanya neno hili kuwa kwamba tamaa alizozimaanisha Yakobo hapa ni tamaa mbaya tu. Lakini ni vyema kudiriki kutafakari zaidi kidogo ya hapo na kufikiri kwamba yawezekana si tu tamaa mbaya huwajaribu watu bali hata tamaa nzuri. Ebu fikiri unapotamani kuendesha gari zuri kama la mtu fulani unayemuona kila unapokwenda kazini. Hii bila shaka ni tamaa ya maendeleo na imeumbwa hivyo moyoni mwa binadamu na Mungu mwenyewe kwa ajiri ya kukusaidia ukue na kuongezeka. Lakini mara adui shetani anapogundua juu ya tamaa yako hiyo, yeye  hukuletea mawazoni kwako njia ambazo waweza kuzitumia kujipatia gari la jinsi hiyo na hata bora kuliko hilo na mara zote njia ambazo ukuonyesha si za halali bali ni zile ambazo ni kinyume na neno takatifu la Mungu.  Ndiposa Yakobo anasema “…huku akivutwa…” maana yake kuna mahala huyu mtu mwenye tamaa amesimama na kuna nguvu inayomvuta kutoka hapo. “…na kudanganywa..” hii ni kusema yeye aliye baba wa uongo huingia kazini kumdanganya mtu huyu ama akitumia watu walio upande wake au akiyashambulia mawazo yake moja kwa moja. Mathayo 4: 2-3. “….mwisho akaona njaa. Mjaribu akamjia…” hapa unaweza kuona jinsi mjaribu alivyochukua hadhari kubwa kusubiri Yesu aone njaa na ndipo akamjia. Wote tunajua kwamba baada ya kufunga kwa siku arobaini, Yesu alikuwa na haki kabisa kuona njaa ila shetani alitaka kuutumia mwanya huo kumtegenezea njia ya mkato katika kufikia hitaji lake la kupata chakula na njia hiyo ya mkato ingekuwa dhambi mbele za Mungu.
(ii)            Majaribu yatokanayo na shetani
Hii ni aina ya majaribu ambayo shetani moja kwa moja anakushambulia kwa lengo la kukutoa kwenye msimamo wako kwa Mungu wako. Bila shaka hii ni aina ambayo imewakumba na kuwaua wengi kiroho. Mathayo 4:8-10 hapa  tunamuona Ibilisi akimjaribu yesu kwenye eneo ambalo Ibilisi mwenyewe na Yesu wanajua kwamba haipaswi kwa mwanadamu kumsujudia mwingine yeyote isipokuwa Mungu peke yake. Ibilisi anatumia mali, mamlaka, hata umaarufu kumshawishi Yesu kwenda kinyume na maagizo ya msingi ya Mungu kwenye uumbaji wake. Kwenye maeneo mengi ya maisha yetu ya Ukristo tumeshindwa kusimamia kweli ile tunayoifahamu kwa ajiri tu ya kupata faida flani ya kidunia na ni hapo shetani alipopata nafasi ya kujitukuza juu ya imani zetu. Fikiri ni wakristo wangapi wameacha misingi ya imani yao kama kufunga na kuomba, kuhudhuria ibada na kadhalika kwa sababu muda huo ni muhimu kwa ajiri ya kufanya shughuli nyingine za kujiongezea kipato. Katika dunia inayoendelea kwa kasi hivi, hali hii huonekana ya kawaida, lakini maandiko yametuonya kabla (Mark 4:19). Kama kuna shida kubwa inayolikabili kanisa kwa ujumla wake na  kila mwamini mmoja mmoja ni kuenenda kwa kawaida ya dunia yaani kusema ni kawaida kwa mambo ambayo dunia husema ni ya kawaida. Vijana wangapi wanafanya kile ambacho Biblia huita uasherati kwa vile ( kwa tafsiri ya kidunia) ni kawaida kwa kijana kuwa na mpenzi wake mradi tu asiwe na zaidi ya mpenzi mmoja kwa wakati mmoja?.
Njia ya pili ambayo shetani amekuwa akiitumia katika kuwajaribu watu ni kwa kutumia dhiki na mateso. Njia hii ilikuwako tangu zamani hata hivyo si mpya Dan 3: 13-23. Ebu waza juu ya vijana watatu ambao kwanza wanaishi uhamishoni kwa sababu ya hali ya kukosekana usalama nchini kwao. Hali hii inaweza isieleweke kwa nchi zile ambazo hazijashuhudia vita hata vya wenyewe kwa wenyewe, lakini kwa nchi ambazo zimepitia uzoefu huu, watu wake wanajua jinsi ilivyo vigumu kutunza utamaduni wenu mkiwa ukimbizini. Taifa la Israel ni taifa ambalo utamaduni wao ulifungwa kwenye Torati na ambayo ilikataza si tu kusujudia sanamu, bali hata kuzitengeneza kwa lengo hilo. Kumb 5:8-10 hapa sasa imejitokeza hali ambayo vijana hawa wanatakiwa kuamua, ikiwa wayatunze maagizo ya Mungu ama wajiokoe na kifo cha kuchomwa moto? Ufunuo 2:10-11.
Yako maeneo mengine ambayo twaweza kujifunza juu ya majaribu yatokanayo na shetani, lakini ni vyema hapa uone tofauti ya msingi iliyoko kati ya jaribu na jaribu kwa vile hi ni sehemu muhimu katika kushinda jaribu lako.
Pana jambo ambalo nafikiri niliweke vizuri hapa, kwenye maisha yetu kama wakrsito, nguvu au falme mbili zinashindana katika kutaka kuchukua nafasi ya kwanza kwenye maisha yetu nazo ni ufalme wa giza na ufalme wa nuru. Hivyo ni vyema kufahamu kwamba kila kitu kinachotokea kwenye maisha yako, ufalme wa giza hujaribu kukitumia katika kukuhamisha kutoka ufalme wa nuru. Ashukuriwe Mungu ambaye hufanya kazi katika mambo yote katika kuwapatia mema wale wampendao.
Ni muhimu hata hivyo kufahamu kwamba pana tofauti wakati shetani anapojaribu kutumia tamaa zako mwenyewe kukuondoa katika  mahusiano yako na Mungu, hapo ndipo unapojaribiwa kwa tamaa zako mwenyewe. Wakati shetani anapokukabili moja kwa moja na kukutaka ufanye maamuzi ya kumfuata (kumwabudu), hapo ndipo unapojaribiwa na shetani. Japo shetani ndiye hutujaribu pia wakati tamaa zetu zinapohusika.
Pana nyakati pia ambapo shetani hutushawishi kutumia nafasi ama vipaji vyetu katika maisha kufanya jambo ambalo siyo tu litakuwa kinyume na mapenzi au maelekezo ya Mungu kwenye maisha yetu, bali pia jambo hilo ama litakinzana na sheria za nchi au sheria zinazosimamia nafasi tulizo nazo katika jamii. Mathayo 4:5-7. 1 Sam 24:1-7. Daudi alipata mara mbili nafasi ya kumuua adui yake Sauli ambaye ndiye hasa alikuwa kikwazo cha Daudi kuwa mfalme kama alivyokuwa ametabiriwa na Samweli. Kwa mtizamo wa kawaida, Daudi alipaswa kumpiga Sauli na kumuua na kisha kutafuta njia yake kwenye ikulu ya Israel, lakini Daudi aliugundua haraka mtego wa shetani uliokuwa mwenye kitendo cha Sauli kuingia kwenye mavizio yake. Kulikuwa na sheria iliyokataza mtu yeyote kwa sababu yoyote kumtendea kwa hila mpakwa mafuta wa Bwana, na hapa shetani alikuwa akimwekea  Daudi njia rahisi ya kufikia kusudi la yeye kuwa mfalme. Tunasoma “…nao watu wa Daudi wakamwambia , Tazama , hii ndiyo siku ili aliyokuambia Bwana, Angalia, nitamtia adui yako mkononi mwako, nawe utamtenda yoyote utakayoona kuwa mema”. (1 Sam 24:4). Kumbuka kwamba Daudi alikuwa akiongoza kile ambacho wanasiasa wa karne ya ishirini na moja wangekiita  jeshi la waasi, na hapa wawili labda watano wa makamanda wake, bila shaka ambao waliweza kuongea na kumshauri Daudi, wanampa ushauri sahihi kwa mujibu wa hali halisi ya kisiasa na labda ya kijeshi na kivita lakini siyo kiroho.
Jambo hili linajitokeza tena mara ya pili, 1 Sam 26: 5- 12 na unaona jinsi ambavyo Daudi anaendelea kusimamia imani yake zaidi ya uhalisia wa mazingira yanayomkabili kwa wakati huo. “Ndipo Abishai akamwambia Daudi, Mungu amemtia adui yako mkononi mwako leo, basi, niache nimpige kwa hilo fumo hata nchi kwa pigo moja, sitampiga mara ya pili. Lakini Daudi akamwambia Abishai, Usimwangamize; kwani ni nani awezaye kuunyosha mkono wake juu ya masihi wa Bwana na asiwe na hatia?” 1Sam 26: 8-9.
Ona ambavyo hata katika huduma ya kanisa twaweza kujaribiwa kuipita mipaka tuliyowekewa na kutaka kufanya huduma zote sisi kinyume na agizo la Mungu. 2 Nyakati 26:16-20. Uzia, mfalme ambaye alikuwa amesimama na Mungu kwa sehemu kubwa ya utawala wake, alikuwa ameshindwa kuigundua mbinu ya shetani hata akajikuta ameongozwa na kiburi cha kuwadharau wengine kwenye taifa la Mungu kwa wito wao na kuingia hekaluni kufukiza uvumba. Mungu akampiga kwa ukoma.

 (iii) Majaribu yatokanayo na Mungu.
Wakristo wengi huamini kwamba Mungu huwa hamjaribu mtu, Uko pia mstari wa Biblia ambao ni kama unaunga mkono mtizamo huo. Yak 1:13 “Mtu ajaribiwapo asiseme, Ninajaribiwa na Mungu; …” Watu wengi wameuchukua mstari huu na kudai Mungu huwa hamjaribu mtu bila kusoma sehemu ya mwisho ya mstari huu isemayo “…maana Mungu hawezi kujaribiwa na maovu, wala yeye mwenyewe hamjaribu mtu” Hii ni kusema, kuna jinsi ambavyo Mungu aweza kumjaribu mtu isispokuwa siyo kwa maovu.
Mwanzo 22: 1 husema juu ya Mungu kumjaribu Abrahamu inaposema “Baada ya mambo hayo, Mungu alimjaribu Abrahamu…” Hii ni kusema Mungu humjaribu mtu kwa sababu na njia tofauti kila mara lakini kwa nia na lengo jema. Majaribu yatokanayo na Mungu huwa na sifa tofauti na majaribu mengine kwa sababu hulenga zaidi kuboresha mahusiano yetu na Mungu na mara zote yana lengo la kutufaidia wenyewe au jamii yetu. Kwa kusema  kwa usahihi ni kwamba Mungu huruhusu kujaribiwa kwetu kwa kuboresha mahusiano yetu naye na kutufaidisha sisi moja kwa moja ama kwa kutufanya msaada kwa jamii yetu na hivyo kupata ridhiko la ushiriki wetu kwenye maendeleo au faida flani ya jamii yetu. Ni aibu kwamba kwa vizazi vingi sana sasa watu wamekuwa hawamtukuzi Mungu moja kwa moja mbele ya jamii wakati wanapofika kwenye kilele cha mafanikio yao hata kama wanajua kwamba Mungu ndiye aliyewafikisha hapo. Mara zote utawasikia hata Wakristo wakisema tu wanamshukuru Mungu kwa kufikia lengo ama kitu flani katika maisha yao lakini bila kwenda mbali na kueleza jinsi Mungu alivyohusika.  Sivyo alivofanya Yusufu, yeye aliwaambia waziwazi ndugu zake ya kwamba bila kujari alipitia hali gani, Mungu ndiye aliyempeleka mpaka pale alipo kwa ajiri ya watu wake. Mwanzo 45: 5-8. Mungu hakuwa amempleka Yusufu alipofika kwa njia rahisi ama ya mkato bali kwa njia ya kujaribiwa na hata kuonewa na ndugu zake wa damu.
Ni rahisi kufikiri Yusufu alikuwa akijaribiwa na shetani lakini yeye mwenyewe anasema sivyo bali alikuwa akijaribiwa na Mungu. Pia mtunga zaburi anasema alikuwa akijaribiwa na ahadi ya Bwana. Zab 109: 17-19. “ …..hata ulipofika wakati wa Bwana, ahadi ya Bwana ilimjaribu” Kwa maneno mengine mtunga zaburi anatwambia Yusufu alikuwa akijaribiwa na ahadi ya Bwana.

No comments:

Post a Comment