Wednesday, October 23, 2013

UNAWAZA NINI JUU YA BWANA!?.



Katika ulimwengu wa sasa tunaoishi, si rahisi kuwa Mkristo. Si kwa sababu nyingine yoyote isipokuwa tu kwamba vita kati ya falme mbili yaani ufalme wa giza na Ufalme wa Nuru imefikia mahala pa juu kabisa katika historia ya kizazi chetu walau kwa miaka 100 iliyopita.

Tumesoma mara kadhaa juu ya mashujaa wa imani na gharama walizolipa kuufanya Ukristo uendelee kutajwa duniani, lakini kwa miongo kadhaa, imani hii haijakabiliwa na mashambulizi makubwa kama ilivyo sasa.

Imani inashambuliwa ndani na nje. Ndani ya Imani yenyewe, matendo na maneno yetu yaliyo matunda ya mawazo yetu yamekuwa ama kinyume na ukristo wenyewe ama yamekuwa duni kiasi hatusogei mbele kama tulivyopaswa. Mwandishi mmoja katika Biblia anawauliza watu wa kizazi chake kusema “Mnawaza nini juu ya BWANA…..!” na mimi naomba kukiuliza kizazi hiki cha waamini, MNAWAZA NINI JUU YA BWANA?. Hivyo ni lengo la waraka huu kuwaita waamini wote kujihoji swali hili muhimu. Kila mmoja wetu ajiulize “Ninawaza nini juu ya BWANA…?’. 

Mtume Paulo anatuandikia katika Warumi 12:2 kusema “….lakini mgeuzwe kwa kufanywa upya NIA zenu….”, sasa ukisoma neno NIA kwenye Kiswahili waweza kudhani ni kugeuka kwa malengo ama makusudio ya moyo na tafsiri hiyo ni sahihi, lakini andiko hili linasomeka hivi kwenye kiingereza (KJV)
 “…but be ye transformed by the renewing of your mind, that ye may prove what is that good, and acceptable, and perfect, will of God”. Ni kama Paulo mtume anasema “….mfanywe upya akili zenu….” na mkiisha fanywa upya akili zenu, mtatambua yaliyo mema, mazuri na yenye kumpendeza Mungu.

Kwa nini hatushauriwi kugeuzwa roho zetu, mavazi yetu, madhehebu yetu, shule tunazosoma, vyakula tunavyokula, nyumba tunazoishi na kadhalika, lakini tunashauriwa ‘kugeuzwa akili zetu’?.  Tunaandikiwa mahala pengine kusema “Itumieni akili sawasawa na wala msitende dhambi…”.
Ndugu zangu, kama kuna mali ya thamani ambayo Mungu ameiwekeza ndani yako ni akili yako. Wako watu ambao hupima mafanikio na uwezo wa mtu kwa kuangalia kiasi cha mali alizonazo, na wengi wa hao uhusisha umiliki wa mali na uwezo wa kiakili na hili ni kweli. Akili ndiyo nyenzo ambayo Mungu ameiweka ndani ya mtu kumsaidia kuchanganua mambo na uwezo wa mtu kuchanganua mambo huakisi uwezo wa mtu huyo kuhusiana na jamii na mazingira yake na hata kushindana na changamoto zake. 

Sasa usikwazwe ikiwa utadhani kwamba najaribu kupunguza nafasi ya utendaji wa Roho Mtakatifu katika maisha yako ya kila siku, lakini najaribu kukueleza juu ya ukweli kwamba Roho Mtakatifu anayo nafasi yake katika maisha ya Mkristo, lakini pia akili ya mtu inayo nafasi na mchango wake katika maisha ya Mkristo pia na viwili hili vyapaswa kwenda pamoja. 

Sikubaliani na wazo kwamba ukiamka asubuhi unahitaji kumuuliza Roho Mtakatifu aina ya nguo unayohitaji kuvaa kwa siku hiyo, bali unahitaji kutambua mpangilio wa shughuli zako kwa siku hiyo na kuvaa kulingana na hitajio la wakati. Ingekuwa ajabu ikiwa fundi makenika angeingia kazini kwake akivalia suti nadhifu si kwasababu hawezi kufanya kazi akivalia hivyo, bali mahitaji ya kazi yake ni vazi tofauti na hilo. Kadhalika, mwanasiasa ama mfanyabishara anayekwenda kwenye kikao cha kibishara cha kimataifa akiwa amevaa kaptula, siyo kwamba haweza kuendesha kikao kwa ajiri ya vazi lake, lakini mahala na wakati na hata tukio uhusika katika kuamua aina ya mavazi na hilo ni zao la akili. Ni jukumu la akili yako kutambua aina ya tukio, mahala linapofanyika, mazingira ya tukio lenyewe na kadhalika na kuvaa kulingana na hayo unayoyafahamu. 

Kanisa hata hivyo limeacha ama kwa makusudi au bahati mbaya kuwafundisha watu wake juu ya matumizi sahihi ya kipawa hiki chema na hivyo wengi wa wakristo wanamchukulia Mungu kama mwenye kuketi kando na kusubiri waje kwenye majumba ya ibada na kuabudu na hivyo wanaishi maisha yao yote wakipuyanga tu na kisha kukutana na Mungu wao Jumapili, ama wanamtaka Mungu afanye kila kitu kwenye maisha yao na kwa vile hilo haliwezi kutokea, basi wanadhani ama wana kasoro ama dhambi fulani inayomfanya Mungu asijifunue kwao ama yeye ni Mungu asiyejari kabisa maisha yao ya kila siku, lakini tatizo ni jinsi watu hawa wanavyowaza juu ya Bwana. 

Tunafahamu sote kwamba Yesu alikufa ili tuwe huru kutoka utumwa wa dhambi, lakini mara nyingi tunasahau kwamba Bwana wetu Yesu Kristo alipoanza kufundisha na hata alipowafundisha wanafunzi wake kuomba hakuwafundisha kuomba waende kwenye ufalme wa Mungu bali aliwaambia waombe kusema “Ufalme wako uje (hapa duniani), utakacho kifanyike hapa duniani kama huko mbinguni….”.
Kwa hiyo wakati tunapotafakari pamoja juu ya somo hili UNAWAZA NINI JUU YA BWANA? Lengo ni kukuonyesha mambo machache ambayo yamefunuliwa kwangu katika kuwaza kwangu juu ya BWANA.

Tuesday, September 10, 2013

Wakati wa Kujaribiwa: Sura ya Kwanza, Sehemu ya Pili.



(1)  Aina za Majaribu
Majaribu yote hayako kwenye kundi moja tu. Ziko aina kadhaa za majaribu na hapa tutataja aina kuu tatu za majaribu ambazo ni:
(i)              Majaribu yatokanayo na Tamaa  binafsi za mjaribiwa.
Hii ni aina ya majaribu ambayo mjaribu anategemea hali na mazingira yetu kabla hajatujaribu. Yak 1:12- 14.
Pamekuwa na makosa ya tafsiri kuhusu andiko hili ambalo mzee Yohana anatuandikia kutuonya juu ya kujaribiwa na tamaa zetu. Watafsiri wengi wamelifanya neno hili kuwa kwamba tamaa alizozimaanisha Yakobo hapa ni tamaa mbaya tu. Lakini ni vyema kudiriki kutafakari zaidi kidogo ya hapo na kufikiri kwamba yawezekana si tu tamaa mbaya huwajaribu watu bali hata tamaa nzuri. Ebu fikiri unapotamani kuendesha gari zuri kama la mtu fulani unayemuona kila unapokwenda kazini. Hii bila shaka ni tamaa ya maendeleo na imeumbwa hivyo moyoni mwa binadamu na Mungu mwenyewe kwa ajiri ya kukusaidia ukue na kuongezeka. Lakini mara adui shetani anapogundua juu ya tamaa yako hiyo, yeye  hukuletea mawazoni kwako njia ambazo waweza kuzitumia kujipatia gari la jinsi hiyo na hata bora kuliko hilo na mara zote njia ambazo ukuonyesha si za halali bali ni zile ambazo ni kinyume na neno takatifu la Mungu.  Ndiposa Yakobo anasema “…huku akivutwa…” maana yake kuna mahala huyu mtu mwenye tamaa amesimama na kuna nguvu inayomvuta kutoka hapo. “…na kudanganywa..” hii ni kusema yeye aliye baba wa uongo huingia kazini kumdanganya mtu huyu ama akitumia watu walio upande wake au akiyashambulia mawazo yake moja kwa moja. Mathayo 4: 2-3. “….mwisho akaona njaa. Mjaribu akamjia…” hapa unaweza kuona jinsi mjaribu alivyochukua hadhari kubwa kusubiri Yesu aone njaa na ndipo akamjia. Wote tunajua kwamba baada ya kufunga kwa siku arobaini, Yesu alikuwa na haki kabisa kuona njaa ila shetani alitaka kuutumia mwanya huo kumtegenezea njia ya mkato katika kufikia hitaji lake la kupata chakula na njia hiyo ya mkato ingekuwa dhambi mbele za Mungu.
(ii)            Majaribu yatokanayo na shetani
Hii ni aina ya majaribu ambayo shetani moja kwa moja anakushambulia kwa lengo la kukutoa kwenye msimamo wako kwa Mungu wako. Bila shaka hii ni aina ambayo imewakumba na kuwaua wengi kiroho. Mathayo 4:8-10 hapa  tunamuona Ibilisi akimjaribu yesu kwenye eneo ambalo Ibilisi mwenyewe na Yesu wanajua kwamba haipaswi kwa mwanadamu kumsujudia mwingine yeyote isipokuwa Mungu peke yake. Ibilisi anatumia mali, mamlaka, hata umaarufu kumshawishi Yesu kwenda kinyume na maagizo ya msingi ya Mungu kwenye uumbaji wake. Kwenye maeneo mengi ya maisha yetu ya Ukristo tumeshindwa kusimamia kweli ile tunayoifahamu kwa ajiri tu ya kupata faida flani ya kidunia na ni hapo shetani alipopata nafasi ya kujitukuza juu ya imani zetu. Fikiri ni wakristo wangapi wameacha misingi ya imani yao kama kufunga na kuomba, kuhudhuria ibada na kadhalika kwa sababu muda huo ni muhimu kwa ajiri ya kufanya shughuli nyingine za kujiongezea kipato. Katika dunia inayoendelea kwa kasi hivi, hali hii huonekana ya kawaida, lakini maandiko yametuonya kabla (Mark 4:19). Kama kuna shida kubwa inayolikabili kanisa kwa ujumla wake na  kila mwamini mmoja mmoja ni kuenenda kwa kawaida ya dunia yaani kusema ni kawaida kwa mambo ambayo dunia husema ni ya kawaida. Vijana wangapi wanafanya kile ambacho Biblia huita uasherati kwa vile ( kwa tafsiri ya kidunia) ni kawaida kwa kijana kuwa na mpenzi wake mradi tu asiwe na zaidi ya mpenzi mmoja kwa wakati mmoja?.
Njia ya pili ambayo shetani amekuwa akiitumia katika kuwajaribu watu ni kwa kutumia dhiki na mateso. Njia hii ilikuwako tangu zamani hata hivyo si mpya Dan 3: 13-23. Ebu waza juu ya vijana watatu ambao kwanza wanaishi uhamishoni kwa sababu ya hali ya kukosekana usalama nchini kwao. Hali hii inaweza isieleweke kwa nchi zile ambazo hazijashuhudia vita hata vya wenyewe kwa wenyewe, lakini kwa nchi ambazo zimepitia uzoefu huu, watu wake wanajua jinsi ilivyo vigumu kutunza utamaduni wenu mkiwa ukimbizini. Taifa la Israel ni taifa ambalo utamaduni wao ulifungwa kwenye Torati na ambayo ilikataza si tu kusujudia sanamu, bali hata kuzitengeneza kwa lengo hilo. Kumb 5:8-10 hapa sasa imejitokeza hali ambayo vijana hawa wanatakiwa kuamua, ikiwa wayatunze maagizo ya Mungu ama wajiokoe na kifo cha kuchomwa moto? Ufunuo 2:10-11.
Yako maeneo mengine ambayo twaweza kujifunza juu ya majaribu yatokanayo na shetani, lakini ni vyema hapa uone tofauti ya msingi iliyoko kati ya jaribu na jaribu kwa vile hi ni sehemu muhimu katika kushinda jaribu lako.
Pana jambo ambalo nafikiri niliweke vizuri hapa, kwenye maisha yetu kama wakrsito, nguvu au falme mbili zinashindana katika kutaka kuchukua nafasi ya kwanza kwenye maisha yetu nazo ni ufalme wa giza na ufalme wa nuru. Hivyo ni vyema kufahamu kwamba kila kitu kinachotokea kwenye maisha yako, ufalme wa giza hujaribu kukitumia katika kukuhamisha kutoka ufalme wa nuru. Ashukuriwe Mungu ambaye hufanya kazi katika mambo yote katika kuwapatia mema wale wampendao.
Ni muhimu hata hivyo kufahamu kwamba pana tofauti wakati shetani anapojaribu kutumia tamaa zako mwenyewe kukuondoa katika  mahusiano yako na Mungu, hapo ndipo unapojaribiwa kwa tamaa zako mwenyewe. Wakati shetani anapokukabili moja kwa moja na kukutaka ufanye maamuzi ya kumfuata (kumwabudu), hapo ndipo unapojaribiwa na shetani. Japo shetani ndiye hutujaribu pia wakati tamaa zetu zinapohusika.
Pana nyakati pia ambapo shetani hutushawishi kutumia nafasi ama vipaji vyetu katika maisha kufanya jambo ambalo siyo tu litakuwa kinyume na mapenzi au maelekezo ya Mungu kwenye maisha yetu, bali pia jambo hilo ama litakinzana na sheria za nchi au sheria zinazosimamia nafasi tulizo nazo katika jamii. Mathayo 4:5-7. 1 Sam 24:1-7. Daudi alipata mara mbili nafasi ya kumuua adui yake Sauli ambaye ndiye hasa alikuwa kikwazo cha Daudi kuwa mfalme kama alivyokuwa ametabiriwa na Samweli. Kwa mtizamo wa kawaida, Daudi alipaswa kumpiga Sauli na kumuua na kisha kutafuta njia yake kwenye ikulu ya Israel, lakini Daudi aliugundua haraka mtego wa shetani uliokuwa mwenye kitendo cha Sauli kuingia kwenye mavizio yake. Kulikuwa na sheria iliyokataza mtu yeyote kwa sababu yoyote kumtendea kwa hila mpakwa mafuta wa Bwana, na hapa shetani alikuwa akimwekea  Daudi njia rahisi ya kufikia kusudi la yeye kuwa mfalme. Tunasoma “…nao watu wa Daudi wakamwambia , Tazama , hii ndiyo siku ili aliyokuambia Bwana, Angalia, nitamtia adui yako mkononi mwako, nawe utamtenda yoyote utakayoona kuwa mema”. (1 Sam 24:4). Kumbuka kwamba Daudi alikuwa akiongoza kile ambacho wanasiasa wa karne ya ishirini na moja wangekiita  jeshi la waasi, na hapa wawili labda watano wa makamanda wake, bila shaka ambao waliweza kuongea na kumshauri Daudi, wanampa ushauri sahihi kwa mujibu wa hali halisi ya kisiasa na labda ya kijeshi na kivita lakini siyo kiroho.
Jambo hili linajitokeza tena mara ya pili, 1 Sam 26: 5- 12 na unaona jinsi ambavyo Daudi anaendelea kusimamia imani yake zaidi ya uhalisia wa mazingira yanayomkabili kwa wakati huo. “Ndipo Abishai akamwambia Daudi, Mungu amemtia adui yako mkononi mwako leo, basi, niache nimpige kwa hilo fumo hata nchi kwa pigo moja, sitampiga mara ya pili. Lakini Daudi akamwambia Abishai, Usimwangamize; kwani ni nani awezaye kuunyosha mkono wake juu ya masihi wa Bwana na asiwe na hatia?” 1Sam 26: 8-9.
Ona ambavyo hata katika huduma ya kanisa twaweza kujaribiwa kuipita mipaka tuliyowekewa na kutaka kufanya huduma zote sisi kinyume na agizo la Mungu. 2 Nyakati 26:16-20. Uzia, mfalme ambaye alikuwa amesimama na Mungu kwa sehemu kubwa ya utawala wake, alikuwa ameshindwa kuigundua mbinu ya shetani hata akajikuta ameongozwa na kiburi cha kuwadharau wengine kwenye taifa la Mungu kwa wito wao na kuingia hekaluni kufukiza uvumba. Mungu akampiga kwa ukoma.

 (iii) Majaribu yatokanayo na Mungu.
Wakristo wengi huamini kwamba Mungu huwa hamjaribu mtu, Uko pia mstari wa Biblia ambao ni kama unaunga mkono mtizamo huo. Yak 1:13 “Mtu ajaribiwapo asiseme, Ninajaribiwa na Mungu; …” Watu wengi wameuchukua mstari huu na kudai Mungu huwa hamjaribu mtu bila kusoma sehemu ya mwisho ya mstari huu isemayo “…maana Mungu hawezi kujaribiwa na maovu, wala yeye mwenyewe hamjaribu mtu” Hii ni kusema, kuna jinsi ambavyo Mungu aweza kumjaribu mtu isispokuwa siyo kwa maovu.
Mwanzo 22: 1 husema juu ya Mungu kumjaribu Abrahamu inaposema “Baada ya mambo hayo, Mungu alimjaribu Abrahamu…” Hii ni kusema Mungu humjaribu mtu kwa sababu na njia tofauti kila mara lakini kwa nia na lengo jema. Majaribu yatokanayo na Mungu huwa na sifa tofauti na majaribu mengine kwa sababu hulenga zaidi kuboresha mahusiano yetu na Mungu na mara zote yana lengo la kutufaidia wenyewe au jamii yetu. Kwa kusema  kwa usahihi ni kwamba Mungu huruhusu kujaribiwa kwetu kwa kuboresha mahusiano yetu naye na kutufaidisha sisi moja kwa moja ama kwa kutufanya msaada kwa jamii yetu na hivyo kupata ridhiko la ushiriki wetu kwenye maendeleo au faida flani ya jamii yetu. Ni aibu kwamba kwa vizazi vingi sana sasa watu wamekuwa hawamtukuzi Mungu moja kwa moja mbele ya jamii wakati wanapofika kwenye kilele cha mafanikio yao hata kama wanajua kwamba Mungu ndiye aliyewafikisha hapo. Mara zote utawasikia hata Wakristo wakisema tu wanamshukuru Mungu kwa kufikia lengo ama kitu flani katika maisha yao lakini bila kwenda mbali na kueleza jinsi Mungu alivyohusika.  Sivyo alivofanya Yusufu, yeye aliwaambia waziwazi ndugu zake ya kwamba bila kujari alipitia hali gani, Mungu ndiye aliyempeleka mpaka pale alipo kwa ajiri ya watu wake. Mwanzo 45: 5-8. Mungu hakuwa amempleka Yusufu alipofika kwa njia rahisi ama ya mkato bali kwa njia ya kujaribiwa na hata kuonewa na ndugu zake wa damu.
Ni rahisi kufikiri Yusufu alikuwa akijaribiwa na shetani lakini yeye mwenyewe anasema sivyo bali alikuwa akijaribiwa na Mungu. Pia mtunga zaburi anasema alikuwa akijaribiwa na ahadi ya Bwana. Zab 109: 17-19. “ …..hata ulipofika wakati wa Bwana, ahadi ya Bwana ilimjaribu” Kwa maneno mengine mtunga zaburi anatwambia Yusufu alikuwa akijaribiwa na ahadi ya Bwana.

Saturday, September 7, 2013

Wakati wa Kujaribiwa: Sehemu ya Kwanza.



Biblia inaeleza wazi kwamba kuna “…wakati kwa kila kusudi chini ya mbingu” Muhubiri 3:1. Ukilisoma andiko hili na kutazama hali ya maisha ya kila siku ya Ukristo, utagundua kwamba kuna wakati maalumu wa kujaribiwa. Luka 22:52-53, Bwana Yesu anawaambia wale waliokuja kumkamata kwa nini hawakuwa na wazo la kufanya hivyo hapo kabla, na anasema ni kwa sababu wakati wao ulikuwa bado. Ukipata nafasi ya kujifunza somo liitwalo “Majira na nyakati za mkristo” utaelewa zaidi kuhusu majira na wakati katika maeneo tofauti ya maisha ya mkristo wakati anaposafiri kwenda mbinguni lakini kwenye somo hili tunaangazia mambo kadhaa kama ifuatavyo:
(1)  Jaribu ni nini?
Watu wengi wamekuwa na tafsiri tofauti kuhusu jaribu, lakini si zote zilizo sahihi kwa mujibu wa maandiko. Wengi wa watu wa Mungu huita kila tatizo au changamoto wanayokutana nayo kwenye maisha kuwa ni jaribu. Tafsri hii si sahihi kwa mujibu wa maandiko. Ebu tazama jinsi ambavyo Biblia inayatofautisha matatizo mengine ya kimaisha na majaribu ya kiimani.
 Jaribu ni kipimo cha Imani. Ebu tuseme jaribu ni mtihani wa imani, maandiko hutuonyesha kwamba Imani huja kwa (hutokana na) kusikia (au kujifunza) neno la Kristo (Warumi 10:17) na hivyo baada ya kuwa umeingia kwenye darasa la imani na kujifunza mambo kadhaa wa kadhaa, huitajika ufanye mtihani ambao siyo tu hupima kiwango cha uelewa wako, lakini huamua ikiwa uko tayari kwa kiwango kingine au bado, maana tunatoka imani hata imani hata tukifikie kimo chake Kristo. Warumi 1:17. Hivyo mengi ya yale tuyaitayo matatizo kwenye maisha yetu kama wafuasi, ni mchakato wa kusogea hatua nyingine zaidi.

Mwanzo 22:1 “Baada ya mambo hayo , Mungu alimjaribu Abrahamu….” Tazama msitari huu unavyoanza kwa kusema ‘baada ya mambo hayo’, ndiyo kusema palikuwa na mambo kadhaa yaliyokuwa yametokea kabla ya Abrahamu kujaribiwa. Ni ngumu kueleweka kwa akili za kibinadamu kwamba baada ya Mungu kuwa amemwita Abrahamu kwenye sura ya 12 ya kitabu cha Mwanzo na Abrahamu akatii, baada ya Mungu kumpa Abrahamu ahadi ya uzao mwingi kwenye sura ya 13,  baada ya Mungu kumpigania Abrahamu kwenye sura ya 14 na Abrahamu kumtolea Mungu fungu la kumi kupitia kwa Melkizedeki, baada ya Mungu kumhakikishia Abrahamu kwamba uzao wake mwenyewe ndiyo utakaomrithi na  hapa naomba niseme wazi kwamba Mungu kumhakikishia Ibrahimu juu ya kurithiwa na uzao wake mwenyewe alikuwa amejibu moja ya vitendawili vikubwa vilivyokuwa vikimkabili Ibrahimu, unaweza kumuona Ibrahim akijaribu ‘kumshawishi’ Mungu akubaliane na Ishmael kuwa mwana wa ahadi kwenye Mwanzo 17:17. Ni kama Ibrahimu anamwambia Mungu “ Unajua hili suala linanishinda hata kulielewa, kwa nini tusimalize tu hili jambo kwa kumtwaa Ishmael awe mwana wa ahadi?”. Jibu la Mungu kwa Ibrahim lilikuwa  kumpa Ibrahim jina la mtoto na “…kwa habari ya Ishmael nimekusikia…..”. Ni kama Mungu akisema, Sawa Ibrahim rafiki yangu, ninaelewa kwamba linakusumbua na kwamba unampenda pia mwanao Ishamel,  “…nimembariki…..”.
 Ndiyo maana Roho Mtakatifu anatuwekea jambo hili kwenye maandiko anaposema “Baada ya mambo hayo, Mungu alimjaribu Ibrahim……” Ibrahim alikuwa ametembea na Mungu ya kutosha kujifunza kwamba Mungu anajari mpaka yale mambo madogo madogo yatuumizayo kwa ndani sana. Yale ambayo hatuna hata maneno ama ujasiri wa kutosha kuyasema mbele za Mungu. Mambo ambayo hatuna hakika kama Mungu mkuu namna hii angependa kusikia hoja hizi kutoka kwetu. Pana nyakati katika maisha ambapo tunajaribu kuwaza kwamba Mungu hajari chochote kuhusu hisia zetu isipokuwa  mapenzi yake tu yatimizwe, basi!. Ibrahim alikuwa amejifunza kwamba Mungu alikuwa si dikteta anayetoa tu amri na mipango yake kwenye maisha yetu, bali Mungu anayejari na ambaye anafanya mambo kutubariki. Ibrahim alikuwa amepata daraja flani la Imani na Baraka na sasa ilikuwa wakati wa Ibrahim kusonga mbele tena.

  Sura ya 22, tunamuona Mungu akimjaribu Abrahamu.  Hapa tunaona mambo mawili makubwa. Moja ni kwamba tangu Abrahamu kuitwa asijue aendako (Waebr 11:8) hadi kupigana vita vya kumkomboa ndugu yake (Mwanz 14:13-16) na hata suala la Abrahamu kukosa mtoto kwa miaka mingi, hayo hayakuwa majaribu, na kama yalikuwa majaribu basi hakujaribiwa na Mungu. Maana Biblia inayaweka kwenye fungu moja ambalo Biblia inaliita “Baada ya mambo hayo…” na ndipo inasema Abrahamu alijaribiwa. Pili ni kwamba katika mambo yote hayo ambayo Abrahamu alikutana nayo, Imani yake haikuwekwa njia panda, haikujaribiwa na ndiposa kila anapovuka hatua flani utamuona Mungu ama akilithibitisha tu agano lake kwa Abrahamu au akitoa maelekezo flani, lakini anapovuka kwenye jaribu unaona Mungu akisema jambo tofauti (Mwanzo 22:12) anasema “…sasa najua kwamba unamcha Bwana…”. Maana yake maelekezo ya Mungu mara hii yaliilenga imani ya Abrahamu na siyo kitu kingine.

Ebu fikiri kwenye maisha yako binafsi, wakati ambapo mawazo yako yanakuambia sasa uko sawa  mbele za Mungu na moyo wako ukitegemea kuona Baraka za Mungu, ndipo wakati huo unapojaribiwa.  Tunasoma kitu kinachofanana na hiki kwenye habari za Yusufu, Mwanzo: 39:1-6b. Kwenye maandiko haya utamuona Yusufu akibarikiwa na kupata kibali japokuwa alikuwa  ameuzwa. Aliachiwa kila kitu na bwana wake hata bwana wake “hakujua habari ya kitu chochote chake, ila hicho chakula alichokula” na mstari wa saba unaanza kwa neno hili “Baada ya mambo hayo….” Maana yake baada ya Mungu kuwa amemuonekania Yusufu namna hii, ulikuwa umefika sasa wakati wa Yusufu kujaribiwa.  Utagundua jinsi ambavyo Yusufu alipitia mambo mbalimbali na si mambo yote hayo yalikuwa majaribu. Utaona jinsi ambavyo Yusufu hakuwa na hofu ya “kumkosa Mungu” katika mambo yote aliyopitia  isipokuwa suala la mke wa Potifa lilitishia mahusiano yake na Mungu, lilimuweka njia panda  ikiwa aamue kutembea na mke wa bosi wake (angepata unafuu flani katika maisha kwa kipindi flani) au amuheshimu Mungu halafu aingie kwenye ugomvi na huyu mama kwa vile kwa vyovyote mke wa Bosi wake angejutia kitendo cha kuzifunua hisia zake kwa mtumishi wake na hivyo angekasirika na Yusufu yamkini alifahamu hivyo.  

Tofauti kati ya Jaribu, Kwazo na Teso.
Labda si rahisi sana kuelezea jaribu vizuri kwa kulitofautisha na magumu mengine tuyapatayo katika maisha hata hivyo hapa chini tutajaribu kutofautisha kati ya Jaribu, Kwazo na Teso kwa sifa za mambo haya matatu.
 Jaribu huilenga imani yako yaani mahusiano yako na Mungu moja kwa moja (Ayubu 1:9) kwa kuleta mambo katika maisha yako ambayo ama yatakufanya umtilie shaka Mungu na ahadi zake, utayari au hata uwezo wa Mungu kuzitekeleza, uhalali wa amri za Mungu kwenye maisha yako na kadhalika. Ona jinsi ambavyo shetani hapa hana shida na mali za Ayubu, bali ni kama anamwambia Mungu, “Nahisi Ayubu anakuheshimu kwa ajiri ya  baraka ulizompa na nina uhakika ukimyang’anya basi atahamia kwenye kambi pinzani na wewe”. Ndiyo maana anasema “…naye atakukufuru mbele ya uso wako” Ona ambavyo Mungu hana mashaka na imani ya Ayubu lakini anamruhusu shetani kwenda na kumjaribu kwenye mali zake zote. Twaweza kujifunza mengi kwenye majaribu ya Ayubu kama tutakavyoona huko mbeleni.
 Kwazo huilenga akili yako kwa kutokeza mambo ambayo ama hayakubaliani na falsafa ama misimamo yako mingineyo katika maisha. Ndiposa Yesu Kristo anawaambia wanafunzi wake kwamba “…makwazo hayana budi kuja…” Luka 17:1-3. anawaambia makwazo ni matokeo ya makosa ya kutokufahamu jinsi ya kuyaweka pamoja mazuri na madhaifu yetu katika maisha na hivyo mara nyingi twakoseana na kughafirishana. Na hivyo mwokozi anatushauri  “…jilindeni, kama ndugu yako akikosa, muonye, akitubu msamehe”. Shida kubwa zilizoko leo, zisingekuwako kama tungejifunza juu ya  kuzungumza na  waamini wenzetu kanisani, wafanyakazi wenzetu mahala pa kazi na hata wenzi wetu kwenye ndoa na familia juu ya mambo ambayo tunadhani hayakuwa sawa walipoyasema ama kuyatenda, tujaribu kuwasikiliza wanapotupa sababu za wao kutenda au kusema hivyo na kwa upendo tuwaonyeshe makosa yao. Hapo bila shaka watatubu na sisi tutawasamehe na makwazo yatakomea hapo. Ni vivyo tunapowakosa wenzetu na wakatueleza makosa yetu, tunatubu na kuwaomba watusamehe na makwazo yanakomea hapo. Ebu tazama Lutu na Abrahamu walivyokwazana na wakamaliza tatizo lao kwa mazungumzo. Mwanzo 12:1-12.

1Sam 30: 1-6 .Habari za Daudi kwenye sura hii zaweza kutufunza vizuri juu ya hili, Daudi na kikosi cha askari wake 600 walikuwa wamekimbilia Gathi ili wakae mbali na Sauli. Inaonekana mfalme wa Gathi alikuwa akimuunga mkono Daudi na hivyo alikuwa amempa mji mmojawapo ili yeye na watu wake waweze kuishi.
Siku moja vita vikalipuka kati ya mfalme wa Gathi na Israel na Daudi akitaka kurudisha fadhila kwa mwenyeji wake akaamua kwenda na jeshi lake kwa ajiri ya kupigana dhidi ya Israel, lakini kwa sababu za kiusalama, washauri wa masuala ya usalama wa serikali ya Gathi hawakutaka Daudi aende nao vitani na hivyo akaruhusiwa kurudi yeye na jeshi lake kwenye mji wao. Walipofika, siyo tu mji haukuwepo bali hata familia ya Daudi na familia za askari wake hazikuwapo, maadui walikuwa wameuvamia mji wakauchoma moto na kuwachukua mateka watu wote na pia kuzichukua mali zote kuwa nyara. Biblia haisemi ni kwa nini hawakuwaua watu wote kama ilivyokuwa desturi ya vita, labda kwa sababu walikuwa hawakukutana na upinzani wowote kwa vile askari hawakumo kwenye mji au lah! Lakini ni vyema kusema, Mungu alikuwa amewaponya watu hawa na kuwalinda wasiuawe na adui. Askari wa Daudi kwa mara ya kwanza wakatishia kuasi, walitaka kumpiga mawe kiongozi wao ambaye wamempenda na kumfuata miaka yote. Wengi wa askari hao walikuwa kwa hiyari yao wenyewe wamemfuata Daudi huko msituni na kujiunga naye wakiwa wameacha nyuma maisha yao ya kawaida kwa hiyari yao, lakini hili lilikuwa nimewakasirisha sana na japo halikuwa kosa la Daudi kwa kile ambacho kinaelezwa kwamba “…kwa kuwa nafsi za hao watu zilighafilika sana….”(KJV). kwa tafsiri nyingine watu hawa walikuwa wamekasirika ama kukwaza, lakini siyo kujaribiwa.

Twaweza pia  kusema, kwazo linalenga  furaha na amani ya moyo. Zab 119:165. Tafsiri ya neno “kuwakwaza” kwenye kiingereza (KJV) inasema “to offend them” inatumia neno ‘offend’  ambalo tafsiri yake ni ‘kosea’ ama ‘umiza kihisia’ ‘finya’ na ambalo linatokana na neno “offense” yaani kosa.

Kwa hiyo makwazo Ni mwitikio wetu Kwa makosa ama yetu wenyewe, au ya wenzetu na matokeo yake kwenye maisha yetu ya kila siku.   
 Teso  ni hali ambayo huruhusiwa kwa upendo na Mungu kwenye maisha yetu kwa ajiri ya kukomesha mambo fulani yasiyopendeza katika maisha yetu. Hii ni ajabu kwamba katika upendo wake, muumbaji wa vitu vyote humtumia mwanadamu teso fulani katika maisha yake ili asiingie katika njia isiyompasa. Zab 119:71, Ayubu 36: 15, Zab  118 :18  . Pia  Mungu huyatumia mateso kututendea kama wana wa Mungu na ni kwa faida yetu wenyewe Ebr 12:10. Pia Mungu hutumia teso kama njia ya kuwafundisha watu (hata wale ambao sio wanaoteswa) juu ya jambo flani la Kimungu Daniel 4-5
Kwa hiyo tumeona mambo kadhaa yanayotofautisha jaribu na changamoto nyingine tuzipatazo katika maisha.
(i)              Kwanza jaribu lina muda wake
(ii)            Pili jaribu linalenga imani yako katika Mungu moja kwa moja
(iii)          Tatu jaribu huja baada ya kuwa  Mungu amejifunua kwa jinsi flani kwako.   
 Tutazungumza suala la Muda wa jaribu huko mbeleni kwa upana zaidi.
  * Kwa hiyo twaweza kusema, Shida (changamoto) yoyote haiwi jaribu hadi imekuweka njia panda, uchague kati ya kumtii Mungu au kuchukua maamuzi mbadala yatakayokuepusha na shida inayokukabili. Mwanzo 39:9b, Daniel 3:14-18, Ayubu 2:9-10, 1Pet 1:7